Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban apongeza uteuzi wa kiongozi mpya wa kanisa Katoliki

Ban apongeza uteuzi wa kiongozi mpya wa kanisa Katoliki

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ametuma salamu za pongezi kwa Kardinali Jorge Mario Bergoglio wa Buenos Aires, Argentina, kwa kuchaguliwa kuongoza kanisa katoliki duniani. Kardinali Bergoglio amechukua jina la Pope Francis wa Kwanza ambapo katika salamu zake, Bwana Ban pia amewapongeza waumini wote wa kanisa katoliki duniani kwa hatua hiyo. Halikadhalika Bwana Ban amesema ni matumaini yake kuwa ushirikiano kati ya Umoja wa Mataifa na Vatican utaendelea chini ya uongozi wa busara wa Baba mtakatifu Francis wa I.

(SAUTI YA BAN)

“Tuna malengo mengi yanayofanana kuanzia kuendeleza amani, haki za kijamii na haki za binadamu na kutokomeza umaskini, njaa, vyote ambavyo ni misingi muhimu ya maendeleo endelevu. Pia tuna mtazamo mmoja kuwa changamoto zote zinazoikumba dunia hivi sasa zaweza kupatiwa suluhu kwa njia ya majadiliano.”

Bwana Ban amehitimisha salamu zake kwa kueleza kuwa ana uhakika ya kwamba Pope Francis wa I ataendeleza mchango ulioachwa na mtangulizi wake Pope Benedict wa XVI wa kuendeleza mashauriano baina ya imani mbali mbali za kidini jambo ambalo ni kitovu cha ushirikiano wa pamoja wa maeneo yaliyostaarabika.