Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wakimbizi wa Syria wanahitaji msaada: Baraza la Usalama lionyeshe umoja: Ban

Wakimbizi wa Syria wanahitaji msaada: Baraza la Usalama lionyeshe umoja: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ambaye yuko ziarani nchini Uturuki, hii leo ametembelea kambi ya Islahiye nchini humo inayohifadhi wakimbizi wa Syria na kuelezea kushtushwa na kuguswa na kwake na simulizi kutoka kwa wakimbizi hao wakiwemo watoto.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya ziara kwenye kambi hiyo iliyoko jimbo la Gaziantep, nchini humo, Bwana Ban ametoa mfano wa watoto wawili wadogo ambao ombi lao ni kutaka amani na usalama ili waweze kurejea nyumbani Syria an kwenda shuleni.

Kutokana na hali hiyo Bwana Ban amerejelea tena wito wake kwa pande zote kwenye mzozo wa Syria kuacha mauaji na ghasia kwa kuwa mapigano hayana manufaa yoyote.

Halikadhalika ameisihi Jumuiya ya kimataifa, hususan Baraza la Usalama kuungana na kuchukua uamuzi thabiti dhidi ya mgogoro wa Syria huku akiwaeleza wakimbizi hao kuwa atahakikisha wanapatiwa mahitaji stahili ya kibinadamu.

(SAUTI YA BAN)

Uturuki inahifadhi zaidi ya wakimbizi Laki Mbili wa Syria ambapo kati yao hao Laki Moja na Elfu Thelathini na Watano wanaishi kwenye kambi.