Tuwe chonjo dhidi ya ubaguzi wa aina yoyote- Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ameonya kuwa chuki inaongezeka duniani akitaka kila mtu kuwa chonjo na chuki dhidi ya wayahudi na ubaguzi mwingine wowote ule.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ameonya kuwa chuki inaongezeka duniani akitaka kila mtu kuwa chonjo na chuki dhidi ya wayahudi na ubaguzi mwingine wowote ule.
Guterres amesema hayo mwishoni mwa juma katika sinagogi moja la wayahudi jijini New York, Marekani akiongeza kuwa ni sharti kuwe na umoja kupinga chuki kugeuzwa jambo la kawaida.
Amekariri kuwa ni sharti kuwakataa wale wanaoshindwa kuelewa kuwa kadri koo, kabila au dini inavyokua, utofauti uonekane kuwa ni chanzo cha baraka na wala sio tishio.
Katika hotuba yake hiyo mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa ametoa mifano kutoka sehemu mbali mbali za dunia ikionyesha kuongezeka kwa vitisho vya Unazi pamoja na makundi yenye mwelekeo kama huo yakijaribu kujigeuza sura yakisema eti ni salama yakitaka fadhila zaidi,huku Guterres akionya kuwa makundi hayo ni hatari.
Katibu Mkuu amekamilisha hotuba yake kwa kuhimiza kila mtu kusimama kidete dhidi ya chuki na hivyo kushirikiana pamoja kujenga dunia ilyio na watu wenye mielekeo tofauti lakini wanaopendana na kuishi kwa pamoja.
Naye kiongozi wa dini ya wayahudi , Rabbi Scheiiner, amesema kuwa kila mtu anahusika na matendo ya kutojali wengine.