Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban apongeza taarifa ya viongozi wa Afrika ya kutaka M23 kusitisha mapigano DRC

Ban apongeza taarifa ya viongozi wa Afrika ya kutaka M23 kusitisha mapigano DRC

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameunga mkono taarifa ya pamoja ya Marais Yoweri Museveni wa Uganda, Paul Kagame wa Rwanda na Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo ya kuwataka waasi wa kikundi cha M23 walioingia na kusonga katika mji wa Goma, huko Mashariki mwa DRC kuacha mapigano mara moja.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa amemkariri Bwana Ban akipongeza hatua hiyo iliyotokana na mkutano wa viongozi hao uliofanyika huko Kampala, Uganda ambapo viongozi hao katika taarifa yao wanataka waasi hao kuacha ghasia na vitisho vya kutaka kuiondoa madarakani serikali ya DRC.

Bwana Ban pia ametaka M23 kuacha mapigano kwa mujibu wa makubaliano ya Kampala na kutekeleza amri ya kuondoka mji wa Goma huku akitaka pande zote husika kwenye mgogoro huo kuendeleza mashauriano yaliyoanza baina ya viongozi wa maziwa makuu ya kushughulikia msingi wa mgogoro huo.

Halikadhalika amesisitiza kuendelea kusaidia viongozi wa Afrika kuhakikisha uwepo wa Umoja wa Mataifa huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kunakidhi changamoto zinazoibuka.

Waasi wa M23 waliingia Goma Jumanne na kitendo chao kimesabababisha raia zaidi ya elfu 60 kukimbia makazi yao.