Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO yasema homa ya manjano yakithiri Darfur: serikali yaomba msaada wa chanjo

WHO yasema homa ya manjano yakithiri Darfur: serikali yaomba msaada wa chanjo

Wizara ya afya nchini Sudan, imelitaarifu shirika la afya duniani, WHO juu ya mlipuko wa ugonjwa wa homa ya manjano kwenye vitongoji 23 vya jimbo la Darfur ambapo hadi Jumamosi iliyopita, kulikuwepo na wagonjwa 329 ikiwemo vifo 97.

WHO imesema maeneo ya kati na kusini mwa jimbo hilo la Darfur yameripotiwa kuwa na wagonjwa wengi zaidi.

Uchunguzi uliofanywa katika maabara ya WHO huko Dakar, Senegal katika sampuli mbili za wagonjwa umebaini kuwepo kwa vijidudu vinavyosababisha homa ya manjano.

WHO inasaidia kampeni za kinga, tiba na elimu kupitia viongozi wa kijamii kwenye maeneo yenye mlipuko.

Serikali ya Sudan imeomba kundi la kimataifa la uratibu wa chanjo dhidi ya homa ya manjano- YF-ICG, kusaidia kampeni ya chanjo ambapo tayari kundi hilo limeidhinisha chanjo Milioni 2.4 zinazotarajiwa kuwasili nchini Sudan siku za karibuni.

Kundi hilo la kimataifa la chanjo linahusisha mashirika ya UNICEF, madaktari wasio na mipaka-MSF, shirikisho la kimataifa la msalaba mwekundu na mwezi mwekundu-IFRC na WHO ambayo ni sekretarieti.