Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Katiba mpya na maoni ya umma zinatoa nafasi nzuri kwa Kenya kulinda misitu yake: UNEP

Katiba mpya na maoni ya umma zinatoa nafasi nzuri kwa Kenya kulinda misitu yake: UNEP

Kenya inafaa kuidakia fursa maalum ilotolewa na katiba yake mpya, pamoja na maoni ya umma ili kukomesha uharibifu wa misitu katika maeneo yake ya maji, ambao husababisha hasara ya dola milioni sabini kila mwaka kwa uchumi wake, na kuweka hatarini asilimia sabini ya vianzo vya maji nchini humo. Hayo ni kwa mujibu wa wajumbe waliohudhuria mkutano wa ngazi ya juu mjini Nairobi.

Zaidi ya wajumbe 200, wakiwemo watunga sera, sekta ya kibinafsi, washirika wa maendeleo, sekta ya kijamii na waangalizi wa kimataifa, wamekuwa wakikutana kwa muda wa siku tatu ili kutafuta njia mwafaka ya kukabiliana na suala hilo, ambalo husababisha hasara kubwa ya kiuchumi, kwa mujibu wa ripoti ya pamoja na Shirika la Mpango wa Mazingira la Umoja wa Mataifa, UNEP na Idara ya Misitu ya Kenya, KFS.

Ripoti hiyo kuhusu mchango wa misitu na mazingira husika kwa uchumi wa Kenya, ilibainisha kuwa misitu huchangia sekta nyingi, kwa kiasi cha asilimia 3.6 ya mapato ya jumla ya kitaifa, na wala si asilimia 1.1 kama ilivyo katika takwimu rasmi kwa sasa.