Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ampongeza Obama kwa kuchaguliwa tena kuongoza Marekani

Ban ampongeza Obama kwa kuchaguliwa tena kuongoza Marekani

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon amemtumia salamu za pongezi kwa Rais Barack Obama wa Marekani kwa kuchaguliwa tena kuongoza nchi hiyo kwa kipindi cha miaka minne na kusema ni matarajio yake kuendelea kufanya kazi na Rais Obama na serikali yake kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Marekani na Umoja wa Mataifa.

Bwana Ban amekaririwa na msemaji wake akieleza kuwa changamoto zilizo mbeleni ni nyingi ikiwemo kumaliza mapigano yanayosababisha umwagaji damu nchini Syria, kurejesha mchakato wa amani wa Mashariki ya Kati, kuendeleza maendeleo endelevu na kushughulikia changamoto zitokanazo na mabadiliko ya tabia nchi.

Amesema Umoja wa Mataifa utaendelea kutegemea ushirikiano wa dhati wa Marekani katika masuala hayo na mengineyo wakati ikijitahidi kukidhi matarajio ya watu duniani kote.