Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi Nne za Afrika kukumbwa na baa la nzige: FAO

Nchi Nne za Afrika kukumbwa na baa la nzige: FAO

Nchi za Algeria, Libya, Mauritania na Morocco zinaweza kukumbwa na baa la nzige wiki chache zijazo kutoka eneo la Sahel Afrika Magharibi na hivyo zimetakiwa kujiandaa kukabiliana na wadudu hao waharibifu.

Tahadhari hiyo imetolewa na Shirika la Chakula na Kilimo duniani, FAO ambapo mtaalamu mwandamizi wa utabiri wa mwelekeo wa nzige katika shirika hilo Keith Cressman amesema wadudu hao wanaotokea Chad, Mali na Niger wakifika nchi hizo wanaweza kuharibu malisho ya wanyama na mazao wakati huu ambapo wanatishia mavuno huko wanakotokea.

Bwana Cressman amesema FAO imeweza kufuatilia na kudhibiti mwelekeo wa nzige kutoka Niger na Chad kwa kupulizia dawa lakini inashindwa kufanya hivyo nchini Mali.

Kwa bahati mbaya mwaka huu Mali inatupa changamoto kubwa. Hali tete ya usalama inakwamisha jitihada za kufuatilia hali ilivyo na kuidhibiti, kote hasa kaskazini mwa mali. Pia kaskani mwa Niger ambako vikosi vya kitaifa vinaweza kufanya kazi kudhibti lakini vinapaswa kusindikizwa na askari wa jeshi kuhakikisha usalama wao. Hivyo maeneo ya kutekeleza kazi zao yanakuwa na ukomo.”

Halikadhalika, FAO imeomba msaada zaidi wa kifedha kufikia lengo lake la dola Milioni 10 kwa ajili ya operesheni za kudhibiti nzige ambapo hadi sasa imepata dola Milioni Moja nukta Nne tu.