Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Askari Sita wa MONUSCO na mkalimani wajeruhiwa Mashariki wa DRC

Askari Sita wa MONUSCO na mkalimani wajeruhiwa Mashariki wa DRC

Askari Sita wa kikundi cha kulina amani cha Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, DRC pamoja na mkalimani mmoja wamejeruhiwa katika shambulio la kushtukiza lililofanyika usiku wa kuamkia Jumatano huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, DRC.

Taarifa ya MONUSCO imesema shambulio hilo katika eneo la Buganza, jimbo la Kivu Kaskazini limetokea wakati watu hao wakiwa na wenzao 12 wakirejea kutoka kwenye doria.

Roger Meece ambaye ni Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na pia Mkuu wa MONUSCO amesema shambulio hilo la makusudi halikubaliki na kwamba watashirikiana na mamlaka za kitaifa nchini DRC kubaini wahusika wa tukio hilo na kuwafikisha mbele ya sheria.

Mwezi Julai mwaka huu, mlinda amani wa Umoja wa mataifa aliuawa katika eneo hilo wakati wa mapigano kati ya jeshi la DRC na kikundi cha waasi cha M23, kikosi ambacho kinajumuisha askari walioasi jeshini mwezi Aprili.