Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama la UM laelezwa mashauriano ya kuboresha MINUSTAH

Baraza la Usalama la UM laelezwa mashauriano ya kuboresha MINUSTAH

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Haiti, Mariano Fernandez leo amelieleza Baraza la Usalama la Umoja huo kuhusu mashauriano yanayoendelea na serikali ya Haiti juu ya mpango wa kuimarisha na kupanga upya shughuli za ujumbe wa kimataifa wa kurejesha utulivu nchini Haiti, MINUSTAH.

Bwana Fernandez, akihutubia kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa mjini New York , Marekani amesema mpango huo unaandaliwa ili uendane na majukumu ya kimsingi ya MINUSTAH.

Amesema hatua zinazotarajiwa kuchukuliwa awali ni kupunguza idara tano za jeshi ambapo nafasi zitachukuliwa na maafisa polisi, kwa maana ya kwamba uwakilishi wa kiraia katika MINUSTAH utapunguzwa na kuhusisha shughuli za operesheni pekee.

Kuhusu vurugu za hapa na pale zinazofanywa na baadhi ya raia wengi wao wanaokabiliwa na hali mbaya ya uchumi, Fernandez amesema wameeleza bayana kuwa amani na ulinzi vinategemea hatua za kuimarisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, mambo ambayo yatatoa matumaini kwa wananchi wa Haiti .