Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vifo zaidi vyaripotiwa nchini DRC huku ugonjwa wa Kipindupindu ukizidi kusambaa

Vifo zaidi vyaripotiwa nchini DRC huku ugonjwa wa Kipindupindu ukizidi kusambaa

Umoja wa Mataifa unasema kuwa hadi sasa watu 192 wameripotiwa kuaga dunia kufuatia mkurupuko wa ugonjwa wa kipindupindi kwenye Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wakati zaidi ya visa 3000 vya ugonjwa huo vikiripotiwa tangu mwezi Machi. Shirika la afya duniani WHO na washirika wengine kwa sasa wanaisaidia serikali kuendesha kampeni za usafi na kuhakikisha walioambukizwa ugonjwa huo wamepata matibabu.

Ugonjwa huo unaripotiwa kusambaa kwenye mikoa ya Equateur, Bandundu na mji mkuu Kinshasa. WHO inasema kuwa huku ugonjwa wa kipindupindu ukiwa si tisho kwa nchi zinazodumisha hali ya juu ya usafi bado unasalia kuwa tatizo kubwa kwa nchi zisizo na maji safi ya kunywa na mazingira yasiyo salama.

Ugonjwa wa kipindupindu husababishwa kwa kunywa maji au kula chakula kilicho na bacteria za ugonjwa huo na husababisha kukauka kwa mwili baada ya mgonjwa kuendesha na unaweza kusababisha kifo kwa haraka ikiwa mgonjwa hatapa matibabu.