Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa haki za binadamu ataka ufanyike uchunguzi wa vifo Tunisia

Mkuu wa haki za binadamu ataka ufanyike uchunguzi wa vifo Tunisia

Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay leo ametoa wito kwa serikali ya Tunisia kuhakikisha kwamba majeshi yake ya ulinzi na usalama yanasitisha matumizi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji.

Pillay pia ametaka ufanyike uchunguzi huru na wa wazi wa vifo vya waandamanaji wakati wa maandamano ya kupinga ongezeko la bei ya bidhaa, ukosefu wa fursa za ajira, ufisadi na kunyimwa kwa haki na uhuru wa watu.

Takwimu rasmi za serikali zinaonyesha kuwa watu waliouawa wakati wa ghasi za Januari 8-9 ni 21 wakati mashirika ya haki za binadamu yakisema ni kubwa zaidi. Maandamano hayo yaliyoanza Desemba 17 bado yanaendelea nchi nzima. Pillay amesema anahofia vifo hivyo vya watu na kutaka misingi ya haki za kimataifa za binadamu izingatiwe nchini Tunisia.