Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kikundi cha wanawake cha Afrika Kusini chatoa mafunzo kwa polisi kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia

Maafisa wakiwa katika picha ya pamoja baada ya warsha ya polisi inayozingatia jinsia nchini Afrika Kusini, Desemba 1, 2023.
UN Women/Asiphe Saul
Maafisa wakiwa katika picha ya pamoja baada ya warsha ya polisi inayozingatia jinsia nchini Afrika Kusini, Desemba 1, 2023.

Kikundi cha wanawake cha Afrika Kusini chatoa mafunzo kwa polisi kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia

Wanawake

Kiwango cha unyanyasaji dhidi ya wanawake na wasichana nchini Afrika Kusini ni miongoni mwa viwango vya juu zaidi duniani: kulingana na takwimu rasmi, mwanamke mmoja kati ya watano walio katika uhusiano amepitia ukatili wa kimwili uliofanywa na mpenzi wake.

Wengi zaidi wameteseka aina nyingine za vurugu kutoka kwa wanaume wanaowajua na watu wasiowajua. Kikwazo kimoja kikuu cha kushughulikia suala hili ni ukweli kwamba matukio mengi ya unyanyasaji hayaripotiwi kwa mamlaka.

Katika baadhi ya matukio, waathiriwa wanasitasita kuripoti unyanyasaji kwa sababu wanahisi kuwa maafisa wa polisi hawajafunzwa vya kutosha kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia na wanaweza kuwa wasiojali au kutojali wasiwasi wao.

Ilitha Labantu

"Tulikuwa tukipata malalamiko kutoka kwa wateja wetu kuhusu jinsi walivyotendewa vibaya katika vituo vya polisi", anasema Ella Mangisa, Mkurugenzi Mtendaji wa kikundi cha kutetea haki za wanawake cha Ilitha Labantu. "Mwanamke anayekimbia hali ya vurugu ataambiwa arudi na kutatua mambo na mnyanyasaji wake au kuambiwa haya ni masuala ya kibinafsi wanayohitaji kutatua wao wenyewe."

"Tulipochimba zaidi, tuligundua kuwa ilikuwa ni ukosefu wa uelewa, usikivu, na ukosefu wa maarifa kwa upande wa maafisa wa mstari wa mbele", Mangisa aliendelea. "Wengi hawakujua nini hasa cha kufanya wakati mwanamke anapokuja kuripoti au jinsi ya kushughulikia manusura katika hali yao iliyo hatarini zaidi."

"Hatimaye tuliamua kuwa badala ya kuripoti mara kwa mara afisa mmoja mmoja kwa matukio haya tunahitaji mbinu pana, yenye msingi wa suluhisho", aliongeza.

Kupitia ushirikiano na Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN Women) na kwa msaada wa serikali ya Ireland, Elma Foundation, na Bread of the World, Ilitha Labantu ilizindua mpango mwaka 2021 wa kufanya kazi na Huduma ya Polisi ya Afrika Kusini (SAPS) kuhusu mbinu inayowalenga waathirika kuwaelekeza maafisa kufanya kazi na waathirika wa ukatili wa kijinsia.

Programu za mafunzo zinahusu mada kama vile kufafanua jinsia, utete wa kijinsia, kanuni hatari za kijamii, suluhu na taratibu za kisheria, jukumu la SAPS, kufanya kazi kwa manusura wa unyanyasaji, kushughulikia watu waliojeruhiwa, na ushauri wa kimsingi.

Kupunguza unyanyasaji dhidi ya wanawake nchini Afrika Kusini kunahitaji "mbinu ya jamii nzima", alisema Aleta Miller, Mwakilishi wa UN Women katika ofisi ya Afrika Kusini inayowakilisha Nchi Mbalimbali.

“Mpango huu unaoongozwa na Ilitha Labantu ni fursa ya kufanyia kazi kuelekeza madawati ya kuripoti Unyanyasaji wa kijinsia katika vituo vya polisi, kuboresha uzoefu wa walionusurika wakati wa kuripoti kesi, na kuhakikisha polisi wanapata mafunzo yanayohitajika ili kukabiliana na ukatili dhidi ya wanawake na wasichana, kukabiliana na ukatili dhidi ya wanawake na wasichana. kwa mahitaji ya wanawake na wasichana,” aliongeza.

 Mpango umekubalika

SAPS imekubali mpango huo, na umetekelezwa katika vituo 75 vya polisi huko Cape Metro na Cape Winelands katika Mkoa wa Cape Magharibi. Mnamo tarehe 1 Desemba 2023, maafisa 66 walihitimu baada ya kukamilisha moduli zote za mafunzo.

Ilitha Labantu inapanga kupanua zaidi mpango huo kote Afrika Kusini, na kuleta mashirika mengine yenye maeneo tofauti ya utaalamu. Shirika hilo pia linatarajia kujumuisha maudhui kutoka kwa mafunzo yake katika mtaala wa vyuo vya polisi nchini.

Mmoja wa washiriki wa mpango huo, Sargent Rudolf Valentyn, afisa wa kuzuia uhalifu wa kijamii, alisema mafunzo hayo yaliwapa maafisa zana za kukabiliana vyema na ukatili wa kijinsia.

"Katika jamii yetu tuna changamoto kubwa na [ukatili wa kijinsia] na katika miezi michache iliyopita nimepata uzoefu na ujuzi mwingi katika kushughulikia haya", alisema. "Tulijifunza kuhusu masuala kama vile unyeti wa kijinsia na kusikiliza vizuri bila kuwahukumu wateja wetu wanapokuja kuripoti. Pia tulijifunza kuhusu hatua tofauti za unyanyasaji na aina tofauti za afua.”

Valentyn alisema maofisa pia wanashirikishana ujuzi wa mafunzo hayo na wenzao na wamejenga mtandao wa kusaidia taarifa hizo katika jeshi la polisi.

Mafaniko

Tangu kuzinduliwa kwa programu, Ilitha Labantu imeona kupungua kwa kiasi kikubwa kwa malalamiko kuhusu vituo vya polisi vya mitaa kutoka kwa wateja wao na shirika sasa linapata rufaa zaidi kutoka kwa polisi wakati maafisa wanahitaji usaidizi katika kesi maalum. Kufuatia ushiriki wao katika mpango huo, vituo kadhaa vya polisi pia vimeunda mazingira ya kukaribisha katika vyumba vya kusaidia waathiriwa.

"Maoni ambayo tumekuwa tukipata kutoka kwa jamii na polisi yamekuwa ya kutia moyo", Mangisa alisema. "Polisi ambao wamepitia mafunzo wanatoa taarifa juu ya jinsi wanavyojua sasa la kufanya tangu mtu aliyenusurika anapoingia kituoni."

"Juhudi hizi zitasaidia sana kuimarisha uhusiano wa kikazi kati ya SAPS na jamii kwa kujenga uwezo na mafunzo ya kuwaelimisha na kuwahamasisha juu ya masuala yanayohusiana na kukomesha ukatili dhidi ya wanawake na wasichana", Miller anasema.

"Kozi hiyo ilinifungua macho", alisema Sargent Petrodene Pietersen, ambaye alishiriki katika mafunzo hayo. "Nimejifunza taratibu za kisheria ambao sikuzingatia sana hapo awali. Pia nimejifunza njia sahihi ya kuwashauri [waathiriwa], kuwafuatilia, na jinsi washauri wanapaswa kuwatendea waathiriwa.”

"Ningependekeza sana mpango huu kwa wenzangu kwani unatunufaisha sisi kama maafisa, waathiriwa, familia zao, na jamii pana zaidi" Pietersen alisema. "Imekuwa ikituwezesha na itatuwezesha kuhudumia vyema jamii zetu."