Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNGA 77 yafunga pazia, Rais wa UNGA78 ala kiapo

Csaba Kőrösi (kushoto) Rais wa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la UN akikabishi rungu la kuongoza mkutano kwa Rais wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN (UNGA78). Kulia kabisa ni Naibu Katibu Mkuu wa UN Amina J. Mohammed
UN /Manuel Elias
Csaba Kőrösi (kushoto) Rais wa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la UN akikabishi rungu la kuongoza mkutano kwa Rais wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN (UNGA78). Kulia kabisa ni Naibu Katibu Mkuu wa UN Amina J. Mohammed

UNGA 77 yafunga pazia, Rais wa UNGA78 ala kiapo

Masuala ya UM

Mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa umekunja jamvi asubuhi ya tarehe 5 Septemba 2023, jijini New York, Marekani kwa Rais wa mkutano huo anayemaliza muda wake Csaba Kőrösi akisisitiza kuwa licha ya mikingamo ya kijiografia, ushirikiano baina ya nchi haukwepeki.

“Uwepo wetu unategemea ushirikiano wetu,” amesema Bwana Kőrösi akigusia hoja kama vile mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa bayonuai, elimu na usawa wa kijinsia kama mambo ambayo yanahitaji ushirikiano ili kusonga mbele kwa pamoja.

“Hebu na tuwekeze fedha pale ambako tumeweka ahadi,” ameongeza huku akizitaka serikali zitafsiri maneno kuhusu maendeleo endelevu kwenda kwenye vitendo kupitia bajeti, sera, kanuni na uwezeshaji.

UNGA77 na vikao vya ngazi ya juu 

Tweet URL

Mkutano huo wa 77 ulianza rasmi tarehe 13 Septemba mwaka jana na ulikuwa na vikao vya ngazi ya juu ukiwemo Mkutano wa UN kuhusu Maji mwezi Machi mwaka huu ambap ulipitisha Mpango wa hatua wa kulinda na kuhifadhi rasilimali hiyo adhimu.

Mkutaho huo pia ulishuhudia kupitishwa kwa maamuzi muhimu kuhusu kupunguza athari za majanga, kuhakikisha haki kwa wote, jamii jumuishi, afya kwa wote na matumizi na uzalishaji endelevu.

Kuzingatia Chata

Bwana Kőrösi  amerejelea nguzo tatu kuu za Umoja wa Mataifa ambazo ni amani na usalama, maendeleo, na haki za binadamu ambapo amehoji iwapo misingi hiyo inazingatiwa kwa kina wakati huu mizozo imeshamiri duniani kote.

“Vita nchini Ukraine – sambamba na mizozo mingine ya kivita 51– lazima vikome, kwa mujibu wa Chata ya UN na sheria za kimataifa” ametangaza Rais huyo wa mkutano wa 77 huku akitoa wito kutokomezwa kwa kuenea kwa matumizi ya silaha za nyuklia.

Majawabu ya kuhimili changamoto za usoni

Bwana Kőrösi ameangazia pia umuhimu wa majawabu ya pamoja ambayo sio tu yanatatua changamoto za sasa, bali pia yanatatua changamoto za siku za usoni.

“Tunafahamu kuwa michakato ya ‘kipekepeke’ au ya jambo moja yataleta majibu ya tatizo moja. Tunahitaji ufadhili wa fedha na ushirikiano wa kimataifa.”

Nyakati zinabadilika

Bwana Kőrösi ametaja umuhimu pia wa vyombo muhimu vya UN likiwemo Baraza Kuu na Baraza la Usalama viwanyiwe marekebisho ili viende na wakati.

“Ndege ya kwanza ya abira aina ya Jet ilibeba abiria 36 na hiyo ilikuwa mwaka 1952. Yalikuwa ni mafanikio makubwa katika maendeleo ya teknolojia. Lakini hii haimaanishi kuwa tunaweza kuitumia sasa itupeleke sayari ya Mars….nyakati zinabadilika, na hili shirika lazima libadilike na wakati,” amesisitiza.

Kiapo cha ofisi

Baada ya hotuba ya Bwana Kőrösi anayemaliza muda wake, lilifuatia tukio la kula kiapo kwa Rais-Mteule wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN Dennis Francis ambapo aliahidi kutekeleza wajibu wake kwa uwezo wake wote.

Kisha Rais Kőrösi alikabidhi rasmi kwa Rais Francis rungu la mwenyekiti wa kikao na kisha mkutano ukamalizika.

Baada ya hotuba ya Bwana Kőrösi anayemaliza muda wake, lilifuatia tukio la kula kiapo kwa Rais-Mteule wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN Dennis Francis ambapo aliahidi kutekeleza wajibu wake kwa uwezo wake wote.

Kisha Rais Kőrösi alikabidhi rasmi kwa Rais Francis rungu la mwenyekiti wa kikao na kisha mkutano ukamalizika.

Naibu Katibu Mkuu wa UN, Amina J. Mohammed akihutubia kikao cha kufungwa kwa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la UN,  UNGA77 tarehe 05 Septemba 2023.
UN /Manuel Elias
Naibu Katibu Mkuu wa UN, Amina J. Mohammed akihutubia kikao cha kufungwa kwa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la UN, UNGA77 tarehe 05 Septemba 2023.

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed, akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu, amempongeza Rais Kőrösi kwa stadi zake za uongozi kwa kipindi cha mwaka mzima uliopita.

Amepongeza Baraza Kuu kwa kuendeleza diplomasia, kuimarisha mazungumzo na mijadala na kwa kufanya kazi kusaka majawabu kwa ajili ya watu na sayari.

“Hebu na tuazimia kutumia Baraza hili kama jukwaa la ushirikiano wa kimataifa, kujenga kuaminiana, utangamano na mshikamano baina ya nchi wanachama, na kuhakikisha tunaumba majawabu yatakayonufaisha watu na jamii duniani kote,” amesema Bi. Mohammed.

Utu wetu wa pamoja

Mchana ukawadia wakati wa ufunguzi rasmi wa UNGA78 ambapo Naibu Katibu Mkuu amesisitiza kuwa Baraza Kuu linawakilisha “utu wetu wa pamoja” na “ahadi zetu za pamoja” kwa amani, maendeleo endelevu na haki za binadamu.

Amewatia shime wajumbe kuwa na matumaini na kushirikiana pamoja ili kurejesha Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs  kwenye mwelekeo sahihi.

“Hebu na tuibuke na majawabu ambayo watu wote wanatarajia na kusongesha maendeleo kwa mustakabali bora zaidi, wenye amani zaidi na kwa sayari yenye afya.”

Rais wa UNGA78: Mshikamano wa dunia

Rais wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN Balozi Dennis Francis kutoka Jamhuri ya Trinidad na Tobago Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
UN Photo/Loey Felipe
Rais wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la UN Balozi Dennis Francis kutoka Jamhuri ya Trinidad na Tobago Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Katika hotuba yake ya uzinduzi, Rais wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Dennis Francis,  kutoka Trinidad na Tobago ametaja vipaumbele vyake vinne wakati wa mkutano huo ambavyo ni : amani, ustawi, maendeleo na uendelevu.

Amekiri kuweko kwa changamoto ngumu zinazokabili dunia ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, mizozo na umaskini ambavyo amesema vinasababisha amani iyoyome, huku migawanyiko ya kijifografia imeibua kutokuwa na matumaini kwa mifumo ya ushirikiano wa kimataifa.

“Kama chombo kikuu cha UN cha kutunga sera, Baraza Kuu lina wajibu mahsusi wa kuhakikisha juhudi zinawekwa ili kusimika mifumo ya ushirikiano wa kimataifa, inayoendana na misingi na maadili ya kwenye Chata ya UN,” amesisitiza.

Ni kwa kuzingatia hilo ameangazia harakati za Baraza za kukabiliana na kura turufu ndani ya Baraza la Usalama la UN akisema hatua hiyo ni mweleke wa uwazi na uwajibikaji kuhusu matumizi ya kura turufu.

Ustawi

Akigusia kipaumbele cha pili, amesisitiza umuhimu wa majawabu yanayotatua changamoto kwenye mizozo na hata baada ya mizozo, akisihi nchi wanachama kuzingatia Ajenda ya Utekelezaji ya Addis Ababa.

“Katika kufanya hivyo, tuchagize mpito kuelekea nishati salama na kuongeza usaidizi kwa miradi ya kuhimili mabadiliko ya tabianchi kwa kuhakikisha fedha za ufadhili kwa tabianchi zinapatikana kwa unafuu,” amesema Bwana Francis.

Maendeleo 

Amesisitiza umuhimu wa SDGs na mkutano ujao wa viongozi kuhusu SDGs mwezi huu wa Septemba akisema ni fursa muhimu kuchochea maendeleo ya malengo hayo.

Bwana Francis amesisitiza pia umuhimu wa mshikamanowa dunia na ushirikiano katika kujenga mifumo ya afya yenye mnepo hasa kwa kuzingatia janga la COVID-19, pamoja na umuhimu wa ufadhili kufanikisha SDGs.

Uendelevu

Bwana Francis amesisitiza uharaka wa kutatua suala la mabadiliko ya tabianchi na upotevu wa bayonuai, akitaja pia umuhimu wa marekebisho ya hatua kwa tabianchi.

“Tunahitaji mapinduzi ya matumizi ya uchumi wa shughuli zitokanazo na bahari na ambayo yatasughulikia na kuleta pamoja shaka na shuku kuhusu maji, tabianchi, upotevu wa bayonuai, ardhi na mmomonyoko wa udongo na uhakika wa upatikanaji wa chakula duniani.”

Amesema hiyo ndio njia pekee ya kuwa na hakikisho la mazingira safi na endelevu kwa watu wote.