Dunia inashuhudia mgogoro wa kihistoria wa chakula huku njaa ikibisha hodi katika milango mingi: OCHA
Dunia inashuhudia mgogoro wa kihistoria wa chakula huku njaa ikibisha hodi katika milango mingi: OCHA
Mratibu wa umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths amesema masuala ya kibinadamu duniani yanakabiliwa na mtihani mkubwa ambao haujawahi kushuhudiwa huku mahitaji yakiongezeka kila uchao duniani kote, migogoro ikipandiana na mamilioni ya watu wakihitaji msaada.
Bwana Griffiths ameyasema hao Riadhi kwenye kongamano la masuala ya kibinadamu akimwakilisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Katika kongamano hilo lililobeba mada “Masuala ya kibinadamu yanayoendelea kwa mwaka 2023 na zaidi" Griffiths amesema “Ulimwengu unakabiliwa na janga kubwa zaidi la chakula katika historia ya sasa, na njaa inabisha hodi katika milango mingi. Haki za binadamu, hasa haki za wanawake, zinakabiliwa na mashambulizi makali katika maeneo mengi, na kuadhibu jamii nzima.”
Griffiths ambaye pia ni mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA maeongeza kuwa “Mvutano ni mkubwa ambapo ukosefu wa haki umeachwa uendelee kwa miongo kadhaa. Nchini Ukraine, vita ya kikatili inakaribia kuingia mwaka wake wa pili. Na leo ni wiki mbili tangu matetemeko ya ardhi huko Türkiye na Syria ambayo yamegharimu maisha ya makumi ya maelfu ya watu na kusababisha uharibifu usioelezeka.”
Mahitaji ya kibinadamu hayaelezeki
Mkuu huyo wa misaada ya kibinadamu amesema “Zaidi ya watu milioni 350 kote ulimwenguni kwa sasa wanahitaji msaada wa kibinadamu. Tunahitaji karibu dola bilioni 54 ili kukidhi mahitaji ya msingi ya walioathirika zaidi miongoni mwao. Lakini uzoefu unaonyesha kwamba tunaweza kutarajia kuongeza karibu nusu ya kiasi hicho.”
Ameendelea kusema kwamba kila mwaka, hesabu yetu ya watu wanaohitaji msaada duniani kote na kiwango cha fedha kinachohitajika vinaongezeka. Griffiths amesema mwelekeo ni dhahiri na kuna sababu tatu kuu za kuchagia hili.
Mosi: kabla vita za zamani hazijaisha mpya zinaanza. Migogoro inaendelea na kuwa ya muda mrefu.
Pili: dharura ya mabadiliko ya tabianchi inawakumba watu walio hatarini zaidi. Tuko kwenye mbio za mara kwa mara ili kupunguza athari zake.
Tatu: Kuporomoka kwa uchumi kulikochochewa kwanza na mshtuko wa COVID-19, kisha na vita ya Ukraine ambako kunasukuma mamilioni ya watu ukingoni mwa umasikini.
Na wakati matukio haya makubwa yanaongezeka, rasilimali zinazohitajika kukabiliana na changamoto hizo haziendani na mahitaji.
Licha ya changamoto hakuna kukata tamaa
Bwana Griffiths amesema “kama wafadhili, mshikamano wetu daima utakuwa na watu tunaowahudumia. Jukumu letu ni kusikiliza jamii na mashirika ya mahali hapo ambao ndio waitikiaji wa kwanza, na mara nyingi wahusika pekee, kwenye mstari wa mbele. Jukumu letu na dhamira yetu ni kwamba hatukati tamaa."
Hata hivyo amesema ili kutekeleza agizo hili, tunahitaji msaada wa kila mtu kwa njia za vitendo na zinazoonekana.
Ameongezea kuwa Ili kumaliza vita na mizozo tunayojua na kukomesha mipya kuzuka, tunahitaji haraka juhudi za kidiplomasia. Na ninawashukuru wote wanaosukuma amani katika ngazi zote.”
Pia amesema masuala mengine ynayohitaji kushughulikiwa ni changamoto ya mabadiliko ya tabianchi kwa sababu kila mafuriko, joto la kupindukia, ukame au kimbunga huaacha janga kubwa la kibinadamu.
“Maamuzi yah atua mujarabu za kupunguza utoanji wa hewa chafuzi yamechelewa, ni lazima tubadili mwelekeo kutoka kwenye mafuta kisukuku na kuingia kwenye nishati jadidifu kwa kasi.” Amesisitiza mkuu huyo wa misaada ya kibinadamu.
Duniani kote watu zaidi ya milioni 222 hawajui endapo watakula mlo unaofuata. Milioni 45 tayari wako kwenye hatihati ya janga la njaa ambapo wengi wao ni wanawake na watoto na idadi hii inatia uchungu sana.
Ili kukabiliana na zahma hiyo ya dharura Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametangaza dola milioni 250 kutoka kwenye fuko la dharura la umoja wa Mataifa CERF.