Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukosefu wa fursa Afrika ‘kivuno’ kwa makundi yenye misimamo mikali

Ukosefu wa fursa za ajira katika maeneo kama Niger (pichani) unasababisha watu wengi kuingia katika makundi ya itikadi kali.
© UN News/Daniel Dickinson
Ukosefu wa fursa za ajira katika maeneo kama Niger (pichani) unasababisha watu wengi kuingia katika makundi ya itikadi kali.

Ukosefu wa fursa Afrika ‘kivuno’ kwa makundi yenye misimamo mikali

Amani na Usalama

Ukosefu wa fursa za ajira ni kichocheo kikubwa cha watu kujiiunga na vikundi vyenye misimamo mikali katika nchi za Afrika zilizo kusini mwa jangwa la Sahara, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo jijini New York, Marekani na shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo duniani, UNDP. 

Ikipatiwa jina Safari kuelekea misimamo mikali Afrika: Njia za utumikishaji na uvunjaji, ripoti inataja vigezo vya kiuchumi kama vichocheo vya watu kutumikishwa na makundi hayo. 

Watu wamekata tamaa 

Ukosefu wa kipato, ukosefu wa fursa za ajira na mbinu za kujipatia kipato kunamaanisha “kuhaha kujinasua kimaisha kunashinikiza watu kuchukua fursa yoyote kutoka kwa mtu yeyote yule,” amesema Achim Steiner, Mtawala Mkuu wa  UNDP , akizungumzia ripoti hiyo. 

Ameongeza kuwa takribani asilimia 25 ya watumikishwa wote kwenye vikundi hivyo walitaja ukosefu wa ajira kama sababu kuu, ilhali asilimia 40 wamesema “wanakuwa kwenye mahitaji makubwa ya kujipatia kipato pale ambapo wanakuwa wametumikishwa na makundi hayo.” 

Eneo la Afrika lililo kusini mwa jangwa la Sahara limekuwa kitovu kipya cha misimamo mikali likiwa na takribani nusu ya vifo vyote vilivyosababishwa na ugaidi mwaka 2022. 

Ripoti hiyo inatokana na mahojiano na takribani watu 2,200 kutoka nchi 8 ambazo ni Burkina Faso, Cameroon, Chad, Mali, Niger, Nigeria, Somalia, na Sudan. 

Kwa maneno yao wenyewe 

Zaidi ya watu 1,000 waliohojiwa ni wafuasi wa zamani wa makundi ya misimamo mikali wakiwa baadhi wamejiunga kwa hiari na wengine walitumikishwa kujiunga. 

Robo ya waliojiunga kwa hiari walitaja ukosefu wa ajira, ikiwa ni  ongezeko la asilimia 92 ikilinganishwa na mwaka 2017 UNDP ilipofanya utafiti wa misimamo mikali. 

Takribani asilimia 48 ya walioajiriwa kwa hiari na makundi hayo waliwaambia watafiti kuwa kunakuweko na tukio linalochochea hadi wanajiunga na makundi hayo. 

Familia ambazo zimeyakimbia makaazi yao kaskazini mashariki mwa Nigeria kwa hofu ya kundi la wanamgambo la Boko Haram, mara nyingi hutafuta hifadhi katika jamii za wenyeji katika mpaka wa Diffa, Niger.
OCHA/Franck Kuwonu
Familia ambazo zimeyakimbia makaazi yao kaskazini mashariki mwa Nigeria kwa hofu ya kundi la wanamgambo la Boko Haram, mara nyingi hutafuta hifadhi katika jamii za wenyeji katika mpaka wa Diffa, Niger.

Unyanyasaji pia ni kichocheo cha kujiunga na makundi 

Kwa waliojiunga na vikundi, asilimia 71 wametaja ukiukwaji wa haki zao za binadamu kuwa sababu, mathalani serikali kukiuka haki zao za binadamu,: amesema Nirina Kiplagat, mwandishi mkuu wa ripoit hiyo ambaye pia ni mshauri wa UNDP katika masuala ya ujenzi wa amani. 

Vitendo vya unyanyasaji wa haki za binadamu ni pamoja na baba mzazi kukamatwa au kaka kutoweshwa na jeshi la usalama la kitaifa. Wengi walitaja sababu hii kuwa kichocheo. 

Kwa mujibu wa ripoit hiyo, shinikizo kutoka kwa familia au marafiki, nalo limetajwa kuwa sababu ya pili ya kuchochea watu kujiunga na vikundi vyenye misimamo mikali, ikiwemo wanawake kuwafuata waume zao kwenye makundi hayo. 

Itikali za kidini ni sababu ya tatu ya kujiunga na imetajwa na asilimia 17 ya waliohojiwa. Hii ni saw ana pungufu kwa asilimia 57 ikilinganishwa na utafiti wa mwaka 2017. 

Majawabu yanayojikita kwenye maendeleo 

Ripoti hii mpya ni sehemu ya mfululizo wa sehemu tatu ikichambua jinsi ya kuzuia misimamo mikali. Inaangazia pia umuhimu wa kuondokana na majawabu ya kuimarisha ulinzi pekee na badala yake kutumia majawabu ya maendeleo ili kuzuia watu kujiunga na makundi hayo, inasema UNDP. 

Inatoa tiwo wa uwekezaji zaidi kwenye huduma za kijamii kama vile ustawi wa watoto, elimu na vile vile ukarabati huduma za maendeleo na ujumuishaji wa watu kwenye jamii. 

Bwana Steiner anasema, “mchanganyiko wenye sumu ulitengenezwa na umaskini, uhohehahe na kukosa fursa ambapo wengi wametaja  hakuna tena utawala wa sheria na hivyo wanageukia vikundi vya msimamo mkali ili kuweka usalama. 

Majawabu ya kukabili ugaidi yanayojikita kwenye usalama mara nyingi ni gharama na ufanisi wake ni mdogo, amesema Bwana Steiner akiongeza ya kwamba uwekezaji nao kwenye mikakati ya kukabili misimamo mikali nao hautoshelezi. 

Vikundi vya kigaidi kama vile ISIS, Boko Haram au Al-Qaeda vimeinuka kutokana na mazingira ya maene oyao, lakini vimeanza kukusanya silaha na kupata ufadhili– na kama huko ukanda wa Sahel, vimeruhusu matawi yao kusaka fedha wao wenyewe. 

Mwanajeshi wa Niger akilinda eneo la kimkakati huko Ouallam, Niger.
UN News/Daniel Dickinson
Mwanajeshi wa Niger akilinda eneo la kimkakati huko Ouallam, Niger.

Hakuna cha kushangaza 

Suala la mienendo ya kisiasa na kijiografia halipaswi kumshangaza mtu yeyote,” amesema Mkuu huyo wa UNDP, kwa maana kwamba nchi hazina tena uwezo wa kutoa hakikisho la utawala wa kisheria na usalama, “kwa hiyo fursa ya watu au makundi mengine kushamiri na kuchipuka inaongezeka kwa kiasi kikubwa na tumeshuhudia hilo nchini Mali, Libya na hata Pembe ya Afrika.” 

Kwa kuzingatia mahojiano, ripoti pia imebainisha vigezo vya watumikishwa kuondoka kwenye vikundi kuwa ni pamoja na kutokidhiwa kwa mahitaji yao ya kifedha au kukosa imani kwa uongozi wa vikundi.  

Soma hapa taarifa ya wapiganaji wa zamani DRC kutoka Rwanda ambao wamerejea nyumbani ili kufahamu kwa nini walijiunga na sababu ya kurejea nyumbani.