Salamu za mwaka mpya wa 2023 kutoka kwa Katibu Mkuu wa UN
Salamu za mwaka mpya wa 2023 kutoka kwa Katibu Mkuu wa UN
“Kila Mwaka Mpya ni wakati wa kuzaliwa upya”, ndivyo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres alivyozianza salamu za mwaka mpya wa 2023 kwenda kwa ulimwengu.
Bwana Guterres kwa njia ya video iliyoandaliwa kwa lugha mbalimbali ameongeza kusema kuwa, “tunafagia majivu ya mwaka wa zamani na kujiandaa kwa siku angavu” na kwamba mwaka 2022, mamilioni ya watu ulimwenguni kote walifagia majivu.
“Kuanzia Ukraine hadi Afghanistan hadi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na kwingineko, watu waliacha magofu ya nyumba zao na Maisha yao katika kutafuta kitu bora zaidi.Ulimwenguni kote, watu milioni mia moja walikuwa wakisafiri, wakikimbia vita, moto wa nyika, ukame, umaskini na njaa.”Amesema Guterres
Mnamo mwaka 2023, tunahitaji amani, sasa kuliko hapo awali.
Bwana Guterres ameiweka amani katika makundi kadhaa akisema:
𝕊𝔸𝕃𝔸𝕄𝕌 ℤ𝔸 𝕄𝕎𝔸𝕂𝔸 𝕄ℙ𝕐𝔸 𝟚𝟘𝟚𝟛
"Tunahitaji amani sasa kuliko hapo awali. Mwaka 2023 tuweke amani moyoni mwa maneno na matendo yetu." - @antonioguterres https://t.co/cjv8hvZI4b
HabarizaUN
Amani baina ya mtu na mwingine, kupitia mazungumzo ya kumaliza migogoro.
Amani na asili na tabianchi yetu, kujenga ulimwengu endelevu zaidi.
Amani ndani ya nyumba, ili wanawake na wasichana waweze kuishi kwa kuheshimiwa utu wao na kwa usalama.
Amani mitaani na katika jamii zetu, na ulinzi kamili wa haki zote za binadamu.
Amani katika sehemu zetu za ibada, kwa kuheshimu imani ya kila mmoja wetu.
Na amani mtandaoni, isiyo na kauli za chuki na matusi.
Mkuu huyo wa UN ameuhitimisha ujumbe wake kwa kutoa wito akisema, “Mwaka 2023, tuweke amani moyoni mwa maneno na matendo yetu. Kwa pamoja, tuufanye mwaka 2023 kuwa mwaka ambapo amani itarejeshwa katika maisha yetu, nyumba zetu na ulimwengu wetu.”