UN yatuma salamu za rambirambi nchini China
UN yatuma salamu za rambirambi nchini China
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametuma salamu za rambirambi kwa serikali ya China, wananchi, na familia ya aliyekuwa rais wa zamani wan chi hiyo Jiang Zemin kufuatia taarifa za kifo chake.
Taarifa iliyotolewa leo jijini New York Marekani na ofisi ya Msemaji wa Katibu Mkuu imemnukuu akieleza kuhuzunishwa sana na taarifa hizo za kifo na kueleza kuwa “Jiang Zemin alikuwa mtetezi thabiti wa ushirikiano wa kimataifa. Utawala wake uliweka alama na maendeleo makubwa ya kiuchumi na taifa la China kujiandikisha kwenye Shirika la biashara la Kimataifa WTO.”
Guterres ameendelea kueleza chini ya uongozi wa Jiang Zemin, China iliandaa Mkutano wa 4 wa kihistoria wa Dunia wa Wanawake mwaka 1995. Mnamo Septemba 2000, alishiriki katika Mkutano wa Milenia wa Umoja wa Mataifa uliofanyika jijini New York.
“Sitasahau kamwe uchangamfu na uwazi wa Jiang Zemin, pamoja na ushirikiano bora niliofurahia nikiwa Waziri Mkuu wa Ureno pamoja naye ili kuhakikisha kuna mpito mzuri wa kuikabidhi China utawala wa Macau,” amesema Guterres.