Guterres akutana na rais wa China mjini Beijing.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amefanya mazungumzo na rais wa China Xi Jingping leo mjini Beijing na kujadili masuala mbali mbali.
Guterres yuko ziarani China kwa ajili ya kuhudhuria mkutano wa siku mbili wa ushirikiano baina ya China na Afrika utakaoanza kesho. Jukwaa hilo la ushirikiano kati ya Mataifa 53 ya Afrika na China lilianzishwa mwaka 2000 baada ya mkutano wa mawaziri uliofanyika mjini Beijing
Mada kuu ya mkutano wa Beijing wa mwaka huu wa 2018 utakaomalizika tarehe 4 September ni ushirika wa ushindi kwa pande zote , kufanya kazi pamoja kwa ustawi wa maendeleo kwa China na Afrika ili kuhakikisha hakuna anayeachwa nyuma.
Mbali ya viongozi mbalimbali wa mataifa na serikali za Afrika kuhudhuria mkutano huo akiwemo pia mwenyekiti wa tume ya Muungan o wa Afrika , mashirika 27 ya kimataifa na ya kanda ya Afrika yatashiriki.
Leo jioni, baada ya kukutana na rais Xi Jinping, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ametembelea makavazi ya Sanaa ya Beijing na bustani ya Beihai.
Bw Guterres aliandamana na Liu Zhenmin, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anaehusika na masuala ya kiuchumi na ya kijamii pamoja na balozi Ma Zhaoxu Mwakilishi wa kudumu wa China katika Umoja wa Mataifa.