Zaidi ya watu 800 wameuawa Mashariki mwa DRC kati ya Februari na Juni 2022- UNHCR
Zaidi ya watu 800 wameuawa Mashariki mwa DRC kati ya Februari na Juni 2022- UNHCR
Hali ya usalama huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC inaendelea kuzorota ambapo shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, linasema mauaji na uporaji wa mali za raia vinaendelea na kwamba kati ya mwezi Februari na mwezi uliopita wa Juni zaidi ya watu 800 wameuawa katika mashambulizi kutoka vikundi vilivyojihami.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi hii leo ,msemaji wa UNHCR Matthew Saltmarch amesema, “tunasikitishwa na tuna wasiwasi mkubwa kutokana na idadi kubwa ya vifo na machungu ya raia ikiwemo raia kulazimishwa kukimbia makwao kutokana na mashambulizi ya kikatili kwenye majimbo ya Mashariki mwa DRC.”
Hali hii haipaswi kuendelea kupuuzwa
Majimbo hayo ni Kivu Kusini na Ituri ambapo akifafanua zaidi amesema kuwa hali hiyo isiyovumilika inaendelea kupanuka na katu haipaswi kuendelea kupuuzwa.
Akichambua takwimu amesema, “mwezi huu pekee mashambulizi ya mfululizo kutoka waasi jimboni Ituri yamesababisha vifo vya watu 11 na nyumba 250 kuporwa mali na kisha kuteketezwa moto. Na Kati ya Februari na Juni mwaka huu UNHCR na wadau wamerekodi zaidi ya vifo vya watu 800 kutokana na mashambulizi ya kutumia silaha na mapanga kwenye jamii mbalimbali jimboni Ituri.”
Cha kusikitisha ni kwamba takribani ya watu 715 kati ya hao waliokufa walikuwa wamesaka hifadih kwenye maeneo ya wakimbizi wa ndani au waliuawa wakati wanarejea nyumbani baada ya kukimbia ghasia.
Zaidi ya watu 20,700 wamefurushwa makwao kutokana na mashambulizi ambayo pia yamechochea uhaba wa chakula jimboni Ituri, jimbo ambalo lina rutuba kubwa na maendeleo yamedumaa kutokana na miongo kadhaa ya mapigano ya kikabila na hivyo kukosesha familia mbinu za kipato.
Makazi ya Kashuga yalisambaratishwa na waasi
Jimboni Kivu Kaskazini, makazi ya wakimbizi wa ndani ya Kashuga yaliyoko mjini Masisi yalisambaratishwa mwezi Juni baada ya watu waliojihami kuvama na kuua watu wanane na wengine saba walijeruhiwa.
Bwana Saltmarsh amesema katika wiki za karibuni mapigano kati ye jeshi la DRC, (FARDC) na waasi wa kikundi cha M23 jimboni Kivu Kaskazini yamefurusha zaidi ya watu 160,000 kwenye maeneo ya Rutshuru na Nyiragongo.
“Kupangwa upya kwa jeshi la serikali kwenye mzozo huu kumejenga ombo la mamlaka na utete wa usalama kwenye majimbo ya Ituri na Kivu Kaskazini. Mashambulizi yaliyoratibiwa vyema na vikundi vya wanamgambo vilivyojihami vinanyanyasa raia kila uchao majimbo ya mashariki,” amesisitiza msemaji huyo.
Mashambulizi yanakwamisha shughuli za UNHCR
Amefafanua kuwa mashambulizi ya kila uchao yanakwamisha operesheni za UNHCR kufikisha misaada kwa jamii zilizo hatarini wakati huu ambapo ombi la shirika hilo la usaidizi kwa DRC limefadhiliwa kwa asilimia 19 pekee kati ya dola milioni 225 zinazohitajika.
“Tunatoa wito kwa wadau wote kukomesha ghasia hizi zisizo na maana ambazo zinalazimu watu kukimbia makwao. Tunatoa wito wa kuheshimiwa kwa sheria za kimataifa za kibinadamu na za usaidizi wa kibinadamu,” amesisitiza.
Zaidi ya watu milioni 5.6 nchini DRC ni wakimbizi wa ndani na hivyo kufanya idadi kubwa zaidi ya wakimbizi wa ndani siyo tu barani Afrika bali pia duniani.