Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zaidi ya asilimia 50 ya hewa ya Oksijeni yatoka baharini lakini bado tunaichafua- Guterres

Matumbawe yaliyobainiwa na jopo la wanasayansi huko Tahiti. Ni mwamba mkubwa zaidi wa matumbawe kuwahi kufahamika.
© Alexis Rosenfeld
Matumbawe yaliyobainiwa na jopo la wanasayansi huko Tahiti. Ni mwamba mkubwa zaidi wa matumbawe kuwahi kufahamika.

Zaidi ya asilimia 50 ya hewa ya Oksijeni yatoka baharini lakini bado tunaichafua- Guterres

Tabianchi na mazingira

Ongezeko la kiwango cha maji ya bahari, kwa joto la maji ya bahari, kiwango cha asidi baharini na kiwango cha juu cha hewa ya ukaa baharini, vinatishia ustawi wa bahari ambayo ni tegemeo la binadamu, amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake hii leo ambayo ni siku ya bahari duniani.

Guterres anasema ripoti ya mwezi uliopitia ya shirika la Umoja wa Mataifa la hali ya hewa duniani, WMO, ilithibitisha kuwa matatizo hayo yanayokumba bahari yanachochewa utatu wa majanga ambao ni; mabadiliko ya tabianchi, kupotea kwa bayonuai na uchafuzi “na sasa afya ya bahari ambayo ni tegemeo letu sote iko hatarini.”

Sehemu ya matumbawe makubwa duniani katika eneo lililoko nchini Australia.
Coral Reef Image Bank/Matt Curno
Sehemu ya matumbawe makubwa duniani katika eneo lililoko nchini Australia.

Katibu Mkuu amesema bahari inazalishaji zaidi ya asilimia 50 ya hewa ya Oksijeni inayotumika duniani na ndio chanjo kikuu cha kipato kwa watu zaidi ya bilioni 1.

“Licha ya utegemezi huo, bado rasilimali za baharini zinatishiwa na shughuli za binadamu. Zaidi ya theluthi moja ya samaki huvuliwa bila utaratibu wa kuzingatia uendelevu. Kiwango kikubwa cha matumbawe kimeharibiwa. Utupaji taka za plastiki umekithiri na kufikia hata visiwa vilivyo ndani zaidi,” amesema Katibu Mkuu.

Nini cha kufanya?

Vishungi vya sigara vinaweza kudhuru maisha ya wanayama majini na kuharibu maji.
Unsplash/Brian Yurasits
Vishungi vya sigara vinaweza kudhuru maisha ya wanayama majini na kuharibu maji.

Katibu Mkuu anasema, ni wakati wa kutambua kuwa ili kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs pamoja na mkataba wa Paris wa mabadiliko ya tabianchi, tunahitaji juhudi za pamoja kukwamua na kuchechemua bahari yetu.

Kusaka mbinu mpya ya uhusiano na bahari yetu. Tushirikiane na mazingira badala ya kupambana nayo. Kujenga ubia jumuishi na maeneo yote duniani, jamii na kusaka mbinu bunifu za kulinda bahari.

Hatua zimeanza kuchukuliwa

Kwa mujibu wa Guterres, hatua tayari zimeanza, mathalani mwezi Novemba mwaka jana wa 2021 huko Glasgow, Uingereza wakati wa mkutano wa kimataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi, wajumbe walitambua dhimay a mifumo anuai ya baharini katika kufanikisha malengo ya kimataifa kuhusu tabianchi.

Mnara wa urefu wa futi 30 uliopatiwa jina "Funga bomba la plastiki" ulioandaliwa na msanii na mwanaharakati kutoka Canada Benjamin Von Wong ukiwe nje ya eneo ambako kulifanyika Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa huko Nairobi, Kenya.
UNEP/Cyril Villemain
Mnara wa urefu wa futi 30 uliopatiwa jina "Funga bomba la plastiki" ulioandaliwa na msanii na mwanaharakati kutoka Canada Benjamin Von Wong ukiwe nje ya eneo ambako kulifanyika Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa huko Nairobi, Kenya.

Mwezi Machi mwaka huu, serikali zilikubaliana kuandaa mkataba mpya wa kuondokana na uchafuzi utokanao na plastiki, bidhaa ambayo inatishia uhai wa viumbe vya baharini.

Baadaye mwezi huu, huko Lisbon, mji mkuu wa Ureno, mkutano wa kimataifa utajikita katika kuongeza kasi ya kuchukua hatua kwa kuzingatia sayansi na ubunifu ili kufanikisha lengo namba 14 la SDGs ambalo linamulika viumbe chini ya bahari.

Mvuvi nchini Kenya ambaye anategemea samaki kama mlo na pia kujipatia kipato
© UNDP/Amunga Eshuchi
Mvuvi nchini Kenya ambaye anategemea samaki kama mlo na pia kujipatia kipato

Guterres anatamatisha ujumbe wake akisema, “kuhakikisha afya ya bahari na bahari yenye tija, ni jukumu letu la pamoja, ambalo tunaweza kutimiza tu iwapo tutafanya kazi pamoja” akisema kuwa, “katika siku hii ya Kimataifa ya Bahari duniani, hebu niwasihi nyote mnaohusika na afya ya bahari mshirikiane kuchechemua upya bahari zetu.”