Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wekeeni vikwazo wanaounga mkono wapiganaji mashariki mwa DRC- Rais Tshisekedi

Rais wa DRC Félix Tshisekedi  akihutubia Baraza Kuu kutoka Kinshasa
UN WebTV
Rais wa DRC Félix Tshisekedi akihutubia Baraza Kuu kutoka Kinshasa

Wekeeni vikwazo wanaounga mkono wapiganaji mashariki mwa DRC- Rais Tshisekedi

Afya

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Félix Tshisekedi amehutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 75 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa akieleza kuwa janga la Corona, COVID-19 ambalo pamoja na kusababisha vifo, limekuwa kizingiti kikubwa kwa harakati mbalimbali duniani.
 

Akihutubia kwa njia ya video kutoka Kinshasa, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, kupitia video iliyokuwa imerekodiwa awali, Rais Tshisekedi ametaja harakati zilizokwamishwa na COVID-19 kuwa ni pamoja na zile za kutokomeza umaskini, kusongesha amani na usalama na kusongesha maendeleo ya kijamii na ulinzi wa mazingira.

Wanafunzi wakiwa darasani nchini DRC,  akiwemo Lovely, (wa 2 kutoka kushoto) na pia wananawa mikono yao mara kwa mara.
UNICEF/Josue Mulala
Wanafunzi wakiwa darasani nchini DRC, akiwemo Lovely, (wa 2 kutoka kushoto) na pia wananawa mikono yao mara kwa mara.

Hata hivyo amesema kuwa pamoja na kukabiliwa na janga hilo, kila nchi imekuwa mstari wa mbele kulinda raia wake na wakati huo huo kushirikiana na mataifa mengine kujifunza au kubadilisha uzoefu wa kukabili janga hilo.

“Mgonjwa wa kwanza wa Corona alipobainika jijini Kinshasa tarehe 10 mwezi Machi mwaka 2020, tulitangaza kuwa ni janga la kiafya la umma nchini lakini baada ya kuunda kikosi kazi cha kiserikali. Hata hivyo uzoefu wetu wa kukabiliana na Ebola umetusaidia kudhibiti ugonjwa huo,” amesema Rais Tshisekedi.

Amesema kuwa harakati za ndani sambamba na zile za kimataifa ikiwemo ushirikiano na wadau wa kimaendeleo na shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO, “zimesaidia kupunguza kiwango cha vifo visababishwavyo na COVID-19 kutoka asilimia 10 mwanzoni mwa janga hilo hadi chini ya asilimia 2.5 leo hii.”

Ametumia hotuba hiyo kusihi taasisi fedha za kimataifa kusamehe madeni bila masharti yoyote, kama njia mojawapo ili nchi maskini ziweze kujijenga upya baada ya COVID-19.

Amani na Usalama mashariki mwa DRC

Akizungumzia amani na usalama mashariki mwa nchi hiyo, Rais Tshisekedi amesema bado kuna masalia ya vikundi vilivyojihami ndani na nje ya nchi ambavyo vinaendeleza mashambulizi na kutia hofu kubwa. “Bado hakuna amani na vikundi hivyo siyo tu vinashambulia askari wetu, bali pia raia na walinda amani wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO ambao wanatupatia misaada mbalimbali ikiwemo vifaa.”

Amesema vikundi hivyo vinatekeleza ukatili mkubwa ikiwemo mauaji na ubakaji hususan Beni, Kivu Kaskazini na Njugu huko Ituri na Rutshuru. 

Walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania walio kwenye kikosi maalum cha kujibu mashambulizi cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO wakiwa lindoni kwenye mlima wa Kalima, Rutshuru.
MONUSCO Forces/FIB-TANZBATT
Walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania walio kwenye kikosi maalum cha kujibu mashambulizi cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO wakiwa lindoni kwenye mlima wa Kalima, Rutshuru.

 

“Tulichokiona kinadhihirisha kuwa vikundi hivi vina fedha za kuwawezesha kuendesha shughuli zao, na fedha hizo zinatokana na uporaji wa maliasili na kuziuza nje ya nchi kupitia mitandao mahsusi na bila shaka kwa msaada wa makundi fulani. Katu hatutaweza kusambaratisha hivi vikundi hadi pale tutakapoweza kusambaratisha mtandao huo na wale wanaowaunga mkono. Tunatoa wito kwa jamii ya kimataifa iweke vikwazo mahsusi vya kulenga makundi hayo na wale wanaowaunga mkono,” amesema Rais Tshisekedi.

MONUSCO kuondoka DRC?

Kuhusu mustakabali wa MONUSCO ni kwamba wakati huu wa maandalizi ya kuondoka kwa MONUSCO, ushirikiano kati ya ujumbe huo na jeshi la serikali uimarishwe ili kuhakikisha ulinzi endelevu wa raia hasa kwenye maeneo ambako bado vikundi vilivyojihami vimejiimarisha.