Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atuma salamu za pole kwa waathirika wa shambulizi la Jumamosi nchini Mali

Picha ya maktaba ikiwaonesha walinda amani kutoka Chad wakifanya doria katika mitaa ya Kidal nchini Mali Desemba 2016
UN Photo/Sylvain Liechti
Picha ya maktaba ikiwaonesha walinda amani kutoka Chad wakifanya doria katika mitaa ya Kidal nchini Mali Desemba 2016

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atuma salamu za pole kwa waathirika wa shambulizi la Jumamosi nchini Mali

Amani na Usalama

Katibu Mkuu wa Umoja wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake hii leo Jumapili na mjini New York Marekani, amelaani vikali shambulizi lililofanyika jana Jumamosi dhidi ya msafara wa mpango wa Umoja wa Mataifa wa kuweka utulivu nchini Mali, MINUSMA uliokuwa ukisafiri kati ya Tessalit na Gao, tukio ambalo liliwaua walinda amani wawili wa Umoja wa Mataifa raia wa Misri.

Taarifa hiyo imesema, “Katibu Mkuu anatuma salamu zake za rambirambi kwa familia zilizopoteza wapendwa wao na pia serikali na watu wa Misri.”

Aidha Katibu Mkuu kupitia taarifa hiyo amekumbusha  kwamba mashambuzi yanayowalenga walinda amani wa Umoja wa Mataifa yanaweza kuunda uhalifu wa kivita chini ya sheria za kimataifa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatoa wito kwa mamlaka ya Mali kutoacha juhudi zozote za kuwatambua na kuwaleta mbele ya  haki wahusika wa uhalifu huu mbaya.” Imesisitiza taarifa hiyo.

Vilevile Stéphane Dujarric, Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema kwamba Bwana Guterres anasisitiza kuwa matendo hayo ya kinyama hayatazuia Umoja wa Mataifa kuendelea kuunga mkono watu na serikali ya Mali katika harakati zao za kutafuta amani na utulivu.

TAGS: MINUSMA, Mali, Antonio Guterres, Walinda amanai, Ulinzi na Usalama