Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto milioni 19 duniani walikuwa wakimbizi ndani ya nchi zao 2019- UNICEF

Mtoto nchini Madagascar akila mlo wake wa mchana.
© UNICEF/UNI302583/Ralaivita
Mtoto nchini Madagascar akila mlo wake wa mchana.

Watoto milioni 19 duniani walikuwa wakimbizi ndani ya nchi zao 2019- UNICEF

Wahamiaji na Wakimbizi

Ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF inakadiria kuwa watoto milioni 19 duniani kote walikuwa wakimbizi wa ndani mwaka 2019, ambapo kati yao hao milioni 12 ni wakimbizi wapya kwa mwaka huo wa 2019. 

Ikipatiwa jina “Kupotea Nyumbani” ripoti hiyo inasema kuwa miongoni mwao hao, milioni 12 ni kwa mwaka 2019 pekee ambapo milioni 3.8 kati yao ni kwa sababu ya mizozo, ilhali milioni 8.2 ni kwa sababu ya hali ya hewa ikiwemo mafuriko na vimbunga.

Ripoti hiyo iliyotolewa jijini New York,  Marekani hii leo, inaangazia hatari na changamoto wanazopata watoto hao na hatua zinazotakiwa kuchukuliwa haraka, hasa wakati huu wa janga la ugonjwa wa virusi vya Corona, COVID-19, ambalo linazidi kuwaweka watoto hao hatarini zaidi.

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF, Henrietta Fore amesema kuwa, “mamilioni ya watoto duniani kote tayari wanaishi bila malezi na ulinzi bora. Janga jipya linapoibuka kama vile COVID-19, watoto hawa wanakuwa hatarini zaidi. Ni muhimu kwa serikali na wadau wa kibinadamu washirikiane ili kuwaweka watoto hawa salama, wakiwa na afya bora, wakisoma na wakilindwa.”

UNCEF inasema kuwa watoto wakimbizi wa ndani wanakosa huduma za msingi na wako hatarini kukumbwa na ukatili, ghasia, unyanyasaji, kusafirishwa kiharamu na hata ndoa za mapema na kutenganishwa na familia zao.

Ripoti inasema kwa watoto wakimbizi wapya milioni 12, milioni 3.8 wanatokana na mizozo, ilhali milioni 8.2 ni kwa sababu ya hali ya hewa ikiwemo mafuriko na vimbunga.

Msingi wa ripoti sasa ni kuangazia hatari na changamoto wanazopata watoto hao na hatua zinazotakiwa kuchukuliwa haraka, hasa wakati huu wa janga la ugonjwa wa virusi vya Corona, COVID-19, ambalo linazidi kuwaweka watoto hao hatarini zaidi.

Hapa ni Kaya nchini Burkina Faso, watoto wakicheza ndani ya hema, ikiwa ni eneo rafiki la kucheza kwa watoto wakimbizi wa ndani waliofurushwa makwao kutokana na mzozo nchini humo.
© UNICEF/UNI280742// Vincent Tremeau
Hapa ni Kaya nchini Burkina Faso, watoto wakicheza ndani ya hema, ikiwa ni eneo rafiki la kucheza kwa watoto wakimbizi wa ndani waliofurushwa makwao kutokana na mzozo nchini humo.

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF, Henrietta Fore amesema kuwa, “mamilioni ya watoto duniani kote tayari wanaishi bila malezi na ulinzi bora. Janga jipya linapoibuka kama vile COVID-19, watoto hawa wanakuwa hatarini zaidi. Ni muhimu kwa serikali na wadau wa kibinadamu washirikiane ili kuwaweka watoto hawa salama, wakiwa na afya bora, wakisoma na wakilindwa.”

Ripoti inasema kuwa “Na hasa wakati wa COVID-19, hali za watoto wakimbizi wa ndani na familia zao zinakuwa mbaya zaidi. Mara nyingi wanaishi kwenye kambi au makazi yasiyo rasmi ambako huduma za msingi kama vile afya, elimu hupatikana kwa taabu,”  imesema ripoti hiyo ya UNICEF ikiongeza kuwa ni vigumu hata kuzingatia suala la kutochangamana.

Ni kwa kuzingatia hali hiyo, ripoti inatoa wito wa uwekezaji wa kimkakati na jitihada za pamoja za serikali, mashirika ya kiraia, sekta binafsi, wasaidizi wa kibinadamu na watoto wenyewe kushughulikia vichocheo vya watoto kuwa wakimbizi wa ndani hususan ukatili, manyanyaso na ghasia.

Halikadhalika UNICEF inatoa wito kwa serikali kuitisha mkutano chini ya jopo la ngazi ya juu la ukimbizi wa ndani lililoundwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres, ili kuchukua hatua mahsusi na uwekezaji katika kutoa ulinzi na kuhakikisha huduma za msingi zinafikia watoto wote wakimbizi wa ndani na familia zao.

 “Watoto na vijana wakimbizi wa ndani wanapaswa kushiriki kwenye mazungumzo na mawazo yao yazingatiwe ipasavyo na wapatiwe fursa ya kuwa sehemu ya suluhisho,”  imetamatisha ripoti hiyo.