Nakaribisha uamuzi wa Rais wa Cameroon kuanzisha majadiliano ya kitaifa:Guterres
Amani na Usalama
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amekaribisha tangazo la rais Paul Biya wa Cameroon la kuanzisha mchakato wa majadiliano ya kitaifa.
Kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake jumanne, Bwana Guterres ameichagiza serikali ya Cameroon kuhakikisha kwamba mchakato huo unakuwa jumuishi na kushughulikia changamoto zinazolikabili taifa hilo la afrika ya Magharibi.
Katibu Mkuu pia ametoa wito kwa wadau wote nchini Cameroon wakiwemo wanaoishi ughaibuni, kushiriki katika juhudi hizo.
Pia amerejelea kuhimiza kwamba Umoja wa Mataifa uko tayari kuisaidia Cameroon katika mchakato huo wa kitaifa wa majadiliano.