Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatuwezi kufikia SDG’s bila kuwajumuisha wahamiaji:Espinosa

Wakimbizi wa Sudan Kusini waliopo nchini Uganda
WFP/Henry Bongyereirwe
Wakimbizi wa Sudan Kusini waliopo nchini Uganda

Hatuwezi kufikia SDG’s bila kuwajumuisha wahamiaji:Espinosa

Wahamiaji na Wakimbizi

Miezi mitatu baada ya kupitishwa kwa mkataba wa kimataifa kwa ajili ya uhamiaji salama, wa mpangilio na wa halali  mjini Marrakesh Morocco, leo  Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa linajadili utekelezaji wa mkataba huo.

Akizungumza katika ufunguzi wa mjadala huo kuhusu uhamiaji wa kimataifa na maendeleo kwenye makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York , Rais wa Baraza Kuu Maria Fernanda Espinosa amesema “Leo hii wajibu wetu mkubwa  ni utekelezaji wa mkataba huo wa kimataifa.”

Katika hilo Bi. Espinosa ametangaza kwamba amewateua wawakilishi wa kudumu wenye Umoja wa Mataifa kutoka Bangladesh na Hispania kwa pamoja kuwezesha mchakato wa kubaini mundo wa “jukwaa la kutathimini uhamiaji wa kimataifa” ambalo litawajibika na kufuatia utekelezaji wa mkataba huo wa kimataifa wa uhamiaji. Na kwa mantiki hiyo ametoa wito kwamba “ushiriki wa kina wa nchi wanachama katika mchakato huu ni muhimu sana ili tuweze kuweka mkakati ambao ni thabiti na unaotekelezeka kwa ajili ya kufuatilia na kujifunza”

Uhusiano baina ya uhamiaji na SDGs

Ameongeza kuwa wakati nchi nyingi zimeshaanza kutekezeza vipengele muhimu vya mkataba huo anazitaka nchi kutoa takwimu sahihi na taarifa za ushahidi zinazoainisha hali halisi ya wahamiaji. “Hebu tusisahau kwamba nyuma ya namba hizo na takwimu ni binadamu, familia na majina yao, hakuna mtu mwingine yeyote atakayeiacha nyuma familia yake, ardhi yake, au urithi wake bila kuwa na sababu ya msingi.”

Espinosa amesema uhamiaji wa kimataifa na maendeleo endelevu ni kama lila na fila, ni mada mbili ambazo kila wakati ziko kwenye ajenda ya kimataifa , Rais huyo ya Baraza Kuu amesema anatumai mkutano whuu utatanabaisha uhusiano dhahiri uliopo na kutegemeana baina ya masuala haya mawili.

Hatuwezi kufikia malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) endapo hatutowajumuisha ipasavyo wahamiaji” Ameongeza kuwa lengo namba 10 kipengele cha 7 linaainisha haja ya kuwezesha uhamiaji salama, wa kawaida na uwajibikaji na kutoa wito wa utekelezaji wa mipango na será za uhamiaji. Hata hivyo amesisitiza kwamba katika maiaka ya karibuni dunia imeshuhudia wimbi kubwa la watu kuhama hali ambayo imesababisha vifo kwa maelfu ya watu.

Kwa mantiki hiyo amesema ni muhimu kujumuisha wahamiaji katika será na hatua zenye lengo la kuongeza fursa za elimu bora, afya, huduma za nyumba na mahitaji ya msingi  pamoja na kujenga jamii jumuishi zenye amani.

Bi. Espinosa amesema kufikia SDGs katika kanda n anchi zote kutapunguza sababu zinazochangia uhamiaji.Kwa mtazamo wake kufikia SDGs ni nyenzo muhimu ya kuzuia uhamiaji.

Wakimbizi na wahamiaji kutoka Venezuela wakivuka mpaka kuingia Comombia mnamo tarehe 16 Oktoba 2018
UNHCR/Santiago Escobar-Jaramillo
Wakimbizi na wahamiaji kutoka Venezuela wakivuka mpaka kuingia Comombia mnamo tarehe 16 Oktoba 2018

 

Zaidi ya nusu ya wahamiaji ni wanawake

Espinosa ametoa wito kwa nchi wanachama kujikita zaidi hususan kwa hali na mahitaji ya wahamiaji wanawake akisema mahitaji yao yanawakilisha zaidi ya nusu ya mahitaji yote ya wahamiaji duniani. Ameongeza kuwa wahamiaji wanawake pia ni zaidi ya nusu ya wahamiaji wote wako katika hatari kubwa zaidi ya ukatili na manyanyaso na kwamba wanawake na wasichana ni asilimia 71 ya waathirika wote wa usafirishaji haramu.

Rais huyo wa Baraza Kuu pia amesisitiza uhusiano baiana ya uhamiaji na será za ajira. Akisema kazi zenye hadhi ni ufunguo wa mafanikio ya SDGs na ni suala la kulipa kipaumbele katika uongozi wake.

Amesema kutafanyika tukio maalumu April 10 kuadhimisha miaka 100 ya shirika la kazi duniani ILO hafla ambayo itaruhusu “itaturuhusu kutathimini maendeleo na mustakbali wa soko la ajira na wahamiaji ni lazima wajumuishwe kwenye tathimini hii” amesisitiza.

Espinosa amekumbusha mchango mkubwa wa wahamiaji katika maendeleo. Akisema fecha zinazotumwa na wahamiaji katika nchi zinazoendelea na mchango wake katika maendeleo ni mkubwa mara tatu zaidi msaada rasmi wa maendeleo kwa nchi hizo.

Kwa mwaka 2017 amesema dola bilioni 600 zilitumwa zikiwemo dola bilioni 450zilizoelekezwa kwenye nchi zinazoendelea. Kwa hiyo ameongeza kuwa wahamiaji wanachangia katika kufikia baadhi ya maelengo ya maendeleo ya ajenda ya mwaka 2030 lkama vile kupunguza umasikini, kutokomeza njaa na kuchagiza masuala ya afya.

Kwa kuongezea asilimia 85 ya kipato cha wafanyakazi wahamiaji kinasalia katika nchi walizoko. Hivyo wahamiaji pia wanachangia katika ukuaji wa uchumi w anchi zinazowahifadhi na kuunda fursa za ajira. Katika dunia hii ya utandawazi na ya kutegemeana suala la watu kuhama lazima lieleweke kama ni fursa  na kama chachu ya maendeleo.