Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vita na ukwepaji sheria lazima vikome Sudan Kusini:UN ripoti

Mwanamke mkazi wa Wau Shilluk Sudan Kusini, mji ambao umeharibiwa na mapigano yaliyosambaratisha makazi, shule na hospitali.
UNICEF/UN0236862/Rich
Mwanamke mkazi wa Wau Shilluk Sudan Kusini, mji ambao umeharibiwa na mapigano yaliyosambaratisha makazi, shule na hospitali.

Vita na ukwepaji sheria lazima vikome Sudan Kusini:UN ripoti

Haki za binadamu

Wakati maelfu ya watu kwa mara nyingine wakifurushwa makwao kwa sababu ya machafuko nchini Sudan kusini , tume ya haki za binadamu kwa ajili ya Sudan Kusini imeitaka serikali ya nchi hiyo na pande zote katika mzozo kuheshimu mkataba wa usitishaji uhasama na kutekeleza mkataba huo mpaya wa amani uliotiwa saini miezi mitano iliyopita.

Wito huo upo katika ripoti ya tatu ya tume hiyo iliyotolewa leo ambayo imebaini kwamba machafuko yanayoendelea na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ikiwemo vitendo vya ubakaji na ukatili wa kingono vinaweza kuwa ni uhalifu wa kivita. Kwa mujibu wa mwenyekiti wa tume hiyo ya haki za binadamu kwa ajili ya Sudan kusini  Yasmina Sooka  tangu mwaka 2017 hadi sasa hali ya ukatili wa kingono imekubwa mbaya zaidi na kwamba “Kuna uthibitisho wa mwenendo wa jinsi gani wapiganaji wanavyoshambulia vijiji, kupora nyumba, kuwachukua wanawake kama watumwa wa ngono na kisha kuchoma nyumba na mara nyingi watu wakiwa  ndani yake.” Ameongeza kuwa ubakaji, ubakaji wa magenge, utekeji na utumwa wa ngono pamoja na mauaji vimekuwa kama ada Sudan Kusini.

Bi. Sooka amesema bila shaka uhalifu huu unaendelea kwa sababu ya ukwepaji sheria ambao unasbabisha kila taratibu kuvunjwa. Andrew Clapham ni mmoja wa wajumbe wa tume hiyo

(SAUTI YA ANDREW CLAPHAM)

“Kumekuwa na ukiukwaji wa haki za binadamu ukiwemo ubakaji unaofanywa na makundi na ukatili wa kingono na tunauchukulia uhalifu huu kuwa kama uhalifu wa kivita na tunaitaka serikali na pande zote kuchukua hatua haraka kutekeleza azimio la mkataba wa amani na kufanya uchunguzi na kisha kuwawajibisha wahusika wa uhalifu huo.”

Ameongeza kuwa ripoti imeorodhesha visa katika eneo la Leer , jimbo la Kusini la Unity ambako vijana zaidi ya 8000 waliandaliwa kwenda kupigana kwa kauli kwamba  “ Nendeni mkachukue ng’ombe kutoka kwa Mayendit, pia watekeni na kuwabaka wanawake warembo mtakaowakuta, na poreni vitu vyao”.

Vijana hao pia waliambiwa kwamba huu ni wakati muafaka wa kulipiza kisasi kwa ajili ya ndugu na jamaa waliowapoteza vitani.

Ripoti pia imesisitiza amani ya kudumua inahitaji uwajibikaji na haki ambayo inahitajika kwa maelfu ya wasudan Kusini. Na pia ripoti inasema tume inatiwa hofu na kuzorota kwa kuanzishwa kwa mkakati wa haki na sheria hususani mahakama maalumu , tume ya ukweli na upatanishi na mamlaka ya ulipaji fidia. Ripoti hiyo itawasilishwa kwenye Baraza la haki za binadamu mwezi Machi mwaka huu.