Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanasayansi wasichana wa Afrika wako mstari wa mbele katika vita ya kuleta usawa wa kijinsia katika sayansi-Antonio Guterres.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akihudhuria mkutano wa sayansi,teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) kuhusu programu za kompyuta.
UN Photo/Antonio Fiorente
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akihudhuria mkutano wa sayansi,teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) kuhusu programu za kompyuta.

Wanasayansi wasichana wa Afrika wako mstari wa mbele katika vita ya kuleta usawa wa kijinsia katika sayansi-Antonio Guterres.

Wanawake

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo hii mjini Addis Ababa Ethiopia amekutana na kuzungumza na wasichana kutoka nchi mbalimbali barani Afrika ambao wanashiriki katika mpango wa kuwafanya kubobea katika programu za kompyuta, mkakati wa unaoratibiwa kwa pamoja kati ya Muungano wa kimataifa wa Mawasilino (ITU) na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya wanawake UN Women.

Wasichana wanaohudhuria kozi hii hujifunza kuhusu dijitali, sayansi na ujuzi wa maendeleo binafsi, pamoja na utaalamu wa biashara ili kujihakikishia uwezo wao wa kifedha. Wanafundishwa kuwa wanaprogramu, wavumbuzi na wabunifu ili waweze kushindana katika tasinia kama vile Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na sayansi. 

Tweet URL

Mpango huu utaendelea mpaka mwaka 2022 na unatarajiwa kuwafikia zaidi ya wasichana 2000 katika kambi 18 za sayansi. 

Bwana Guterres amesema kuwa moja ya matatizo ya msingi duniani ni kuwa nguvu iko mikononi mwa wanaume jambo linalosababisha utamaduni unaotawaliwa na wanaume. Guterres ameongeza kusema kuwa barani Afrika hii ni moja ya sababu za kwa nini ni vigumu kwa wasichana kwenda shule na katika kazi za kiteknolojia tatizo ni kubwa zaidi.

Takwimu za ITU za kuanzia mwaka 2017 zinaonesha kuwa pamoja na viwango vidogo vya mtandao wa intaneti, eneo la Afrika lina pengo kubwa la kijinsia katika masuala ya kidijitali ikilinganishwa na kwingine duniani. Takwimu zilionesha asilimia 18.6 ya wanawake ndiyo wanatumia intaneti ikilinganishwa na wanaume ambao ni asilimia 24 wanatumia intaneti.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amekumbusha wakati wake alipokuwa anasoma uhandisi wa umeme kwamba katika darasa lao la watu 300, msichana alikuwa mmoja tu, “Hili ndilo tunapaswa kulibadili, na hatujafika huko. Tunawahitaji wasichana zaidi kuchukua kozi za teknolojia. Hili ni muhimu. Kama wasichana na wanawake hawatahusishwa zaidi katika kazi za kiteknolojia, uhusiano wa kimamlaka utasalia mikono ya wanaume zaidi.”

Jumatatu hii ya februari 11 ni Siku ya kimataifa ya wanawake na wasichana katika Sayansi, siku ambayo inakuza uelewa wa ukweli kuwa wanawake na wasichana wanaendelea kuachwa katika kushiriki kikamilifu kwenye sayansi na umuhimu wa kuibadili hali hii. Kwa mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa, katika masomo ya ngazi ya juu takribani asilimia 30 pekee ya wanafunzi wa kike ndiyo wanachagua masomo yanayohusiana na sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati. Vile vile takwimu hizo zinabainisha kuwa wanawake watafiti  ni asilimia 30 pekee kote duniani.