Kuondolewa kwa nguvu taasisi huru za haki za binadamu Nicaragua kunasikitisha-OHCHR
Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelet Bachelet ameelezea kutiwa hofu na tangazo la serikali ya Nicaragua la kuamrisha taasisi mbili za haki za binadamu kuondoko nchini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswisi hii leo, msemaji wa Ofisi ya haki za binadamu, Ravina Shmdasani amesema, taasisi hizo ambazo zilianzishwa kwa ushirikiano na serikali ya Nicaragua zimefutiwa vibali na mali zao kuchukuliwa na hivi sasa hakuna taasisi yoyote huru ya haki za binadamu nchini humo.
Bi. Shamdasani amesema kufuatiliwa kwa vyombo huru vya habari, ikiwemo mwishoni mwa wiki jana ambapo vyombo vya habari vilishambuliwa, matokeo ni kuwa na nchi ambapo mashirika ya kiraia yako hatarini kufungwa na mashirika ya kimataifa yanakabiliwa na changamoto ya kuendeleza shughuli zake.
Ofisi ya haki za binadamu imesema vitendo vya serikali ya Nicaragua vinaathiri hatua za kusuluhisha mzozo unaokabili nchi hiyo na kuhatarisha majadiliano yoyote ndani ya nchi na nchi jirani na jumuiya ya kimataifa kwa ujumla ambapo athari zake zinaweza kuwa mbaya zaidi.
Kwa mantiki hiyo ofisi hiyo imesema matumaini yake ni kwamba kutapatikana makubaliano na serikali ili kubadili hali ya sasa.