Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya changamoto CAR, misingi ya amani ya kudumu imewekwa

Maafisa polisi kutoka ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini  Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR wakiwa kwenye doria mjini Bouar nchini humo  katika picha hii ya Agosti 2018
MINUSCA/Hervé Serefio
Maafisa polisi kutoka ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR wakiwa kwenye doria mjini Bouar nchini humo katika picha hii ya Agosti 2018

Licha ya changamoto CAR, misingi ya amani ya kudumu imewekwa

Amani na Usalama

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, leo limekuwa na kikao kuhusu Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR ambapo wajumbe wamepokea ripoti ya Katibu Mkuu wa umoja huo kuhusu utendaji wa ujumbe wa chombo hicho nchini humo, MINUSCA.

Akihutubia wajumbe kwa njia video kutoka Bangui, mji mkuu wa CAR, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu nchini humo na mkuu wa MINUSCA Parfait Onanga-Anyanga, amesema licha ya changamoto zinazoendelea kuikumba nchi hiyo, nchi hiyo imeweka misingi ya amani ya kudumu.

Bwana Onanga-Anyanga amesema “mwelekeo wa amani na maridhiano hautakuwa rahisi na kwamba jamii ya kimataifa ni lazima ishirikiane na serikali ya CAR kuhakikisha kuwa mchakato wa amani unakuwa jumuishi na haukwami.

Amesisitiza umuhimu wa kuweka mazingira yatakayopatia fursa ya kufanikiwa mfumo wa Afrika wa kuleta amani akimaanisha kuwa “hii inamaanisha kuwa pande zote husika zishiriki kwenye mazungumzo kwa nia ya dhati na nia njema ili mazungumzo yawe na mafanikio.”

Halikadhalika Bwana Onanga-Anyanga amesema ni vyema kuwa Baraza la Usalama liwe na msimamo mmoja kuhusu mchakato wa amani CAR sambamba na nchi jirani na jamii ya kimataifa kwa ujumla.

Walinda amani wa Umoja wa Mataifa wakati wa uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara mjini Bangui , mji mkuu wa CAR mwezi Septemba mwaka 2014. Mradi huo wa ujenzi uliendeshwa na walinda Amani wa Indonesia kwa ushirikiano na wahandisi wa wizara ya ujenzi ya
Picha na UN/Catianne Tijerina
Walinda amani wa Umoja wa Mataifa wakati wa uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara mjini Bangui , mji mkuu wa CAR mwezi Septemba mwaka 2014. Mradi huo wa ujenzi uliendeshwa na walinda Amani wa Indonesia kwa ushirikiano na wahandisi wa wizara ya ujenzi ya

Akizungumza kwenye mkutano huo, Koen Vervaeke, ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya masuala ya Afrika kwenye Muungano wa Ulaya amesema ni muhimu kwa pande zote kinzani CAR zikajikita katika mchakato wa amani na maridhiano na kwamba, “suluhu ya mzozo unaoendelea ni kupitia  nchi za mazungumzo na si kijeshi.”

Bwana Vervaeke ameongeza kuwa Muungano wa Ulaya kwa upande wake umeazimia kuendeleza ushiriki wake wa dhati kusaidia CAR.

Mzozo kati ya waumini wa kikristho na kiislamu ulianza huko CAR mwaka 2013 na baada ya kupungua kidogo mwaka 2015 ulirejea tena mwaka 2016 na kusababisha ghasia kuenea nchini humo.

MINUSCA ilipelekwa nchini humo mwaka 2014 ikiwa na mamlaka ya kulinda raia, kusaidia kipindi cha mpito cha kisiasa na usambazaji wa misaada ya kibinadamu sambamba na upokonyaji wa silaha na kujumuisha wapiganaji kwenye jamii.