Nchini Syria watoto hawajui maana ya amani- UN
Zaidi ya watoto 7,000 wamepoteza maisha yao au wamejeruhiwa na kuachwa na ulemavu wa kudumu kutokana na mgogoro unaoendelea nchini Syria.
Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto walio kwenye mizozo, Virginia Gamba, amesema hayo leo akihutubia Baraza la Usalama la umoja huo jijini New York, Marekani.
Bi. Gamba amesema watoto hao wamenyanyaswa kwa muda mrefu na pande zote kinzani kwenye mzozo huo uliodumu kwa miaka nane sasa na watoto hao hawafahamu amani ni nini.
(SAUTI YA VIRGINIA)
“Huu ndio wakati kwa watoto wa Syria kuwa na imani katika mustakbala wao na pia kujifunza kuhusu amani ni nini. Na huu ndio wakati kwa watoto hao kujeresha utoto wao waliopokonywa na huu ndio wakati wa watoto kukomesha kitendo cha wao kuwa waathirika.”
Bi Gamba amesema kuwa tangu mwanzo wa mgogoro huo mwezi Machi mwaka 2011, Umoja wa Mataifa umethibitisha visa vya zaidi ya watoto 7,000 kuuawa au kuachiwa umelavu wa kudumu.
Amesisitiza kuwa idadi hiyo ni ile tu ambayo imethibitishwa akiongeza kuwa ripoti ambazo hazijathibitishwa zinatoa idadi ya watoto walioathiriwa katika mgogoro huo kufika 20,000.
Amesema kuwa watoto hao wameteseka na kunyanyaswa kupindukia ikiwemo makwao, kijamii, shuleni, vituo vya kizuizi na pia katika kambi za wasio na makazi.
Bi. Gamba amesema haki za watoto zilikiukwa akirejelea mfumo wa ufuatiliaji na utoaji wa taarifa uliopitishwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, mwaka 2005 au MRM.
Mfumo huo ulioangazia maeneo sita ya ukiukwaji wa haki za watoto kwenye maeneo yenye mizozo ulianza kutekelezwa mwaka 2013 nchini Syria baada ya baraza hilo kupitisha azimio.
Maeneo hayo ni kuua na kujeruhi kunakoacha ulemavu wa kudumu, , kusajili watoto vitani, unyanyasaji wa kingono, utekaji wa watoto, kushambulia shule au hospitali na pia kuwanyima msaada wa kibinadamu.
Wajumbe pia walipata maelezo kutoka kwa mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya binadamu, OCHA, Mark Lowcock ambaye aliweka bayana hali ya kibinadamu nchini Syria akisema nchi ihyo imekumbwa na vita karibu kila mahali.
(SAUTI YA MARK LAWCOCK)
“ Tangu Novemba 2017 idadi ya watu wanaohitaji msaada wa kibinadamu maeneo ya Aleppo na Idlib imeongezeka kwa takriban watu 600,000 na kufikia jumala ya watu milioni 4.2. Na nusu ya watu hao wanahitaji msaada wa haraka kutokana na kutokuwa na makazi, chakula, maji pamoja na mahitaji mengine muhimu.”
Pia amebaini kuwa ombi la mwaka huu la msaada kwa Syria limepata pesa chache na kuongeza kuwa kasi ya kukabiliana na matukio sehemu hiyo inategemea msaada kutoka nchi wanachama na wahisani.