Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tusipopima na kutibu haraka homa ya ini tutakuwa na mtihani mkubwa -WHO

Upimaji wa homa ya ini Togo
UN
Upimaji wa homa ya ini Togo

Tusipopima na kutibu haraka homa ya ini tutakuwa na mtihani mkubwa -WHO

Afya

Mataifa yote duniani yametolewa wito wa  kuongeza  huduma za haraka za upimaji  na matibabu dhidi ya homa ya ini ili kufikia malengo ya afya yaliyokubaliwa duniani.

Wito huo umetolewa  na shirika la afya duniani, WHO pamoja na washirika wake katika kuelekea siku  ya homa ya ini  duniani  inayoadhimishwa kila mwaka Julai 28. Kauli mbiu ya  mwaka huu ni : Pima, Tibu, homa ya ini.

WHO inasema  homa ya ini aina ya B na C huathiri  watu milioni 325 duniani na ikiwa vidudu vyake  havitibiwi haraka vinauwezo wa  kusababisha saratani ya ini ambavyo viliuwa watu zaidi ya milioni 1.3 mwaka 2015 pekee.

 

Pima,Tibu, homa ya Ini

Akizungumzia homa hiyo mkurugenzi mkuu wa WHO, Dr. Tedros Adhanom Ghebreyesus, amesema “tuna mtazamo thabiti wa  kuutokomeza ugonjwa huo na nyenzo tunazo,  lakini ni lazima tuchapuze mchakato ili kufanikisha  lengo hilo ifikapo mwaka wa 2030.”

 Takwimu za WHO zinaonyesha kuwa asilimia 20  tu ya watu ndio  walipata  huduma za kupimwa na kutibiwa dhidi ya   maambukizi ya homa ya ini aina B na C mwaka 2016.

Naye mkurugenzi wa WHO anaehusika na VVU na homa ya Ini, Dr. Gottfried Hirnschall, amesema ili kuweza kutokomeza kabisa  homa ya Ini kutahitajika ubunifu mkubwa, dawa bora na huduma bora za afya.

Siku ya homa ya ini itaadhimishwa kimataifa mwaka huu nchini Mongolia taifa ambalo lina idadi kubwa ya wagonjwa wa homa hiyo duniani.

 

Chanjo dhidi ya homa ya Ini aina ya B Argentina
Photo: WHO/PAHO
Chanjo dhidi ya homa ya Ini aina ya B Argentina

 

 Zaidi ya asilimia 10 ya watu milioni 3  wa Mongilia wanaishi na viini vya homa ya Ini. Taifa hilo lilianza mpango wa kitaifa kukabiliana na ugonjwa wa homa ya ini mwaka 2017 kwa lengo la kuutokomeza kabisa ungojwa huo ifikapo mwaka 2020 .

Taifa hilo linalenga kutoa huduma ya upimaji wa homa ya ini aina B na C kwa asilimia 60 hadi 80 ya watu wake na kutoa tiba ya homa ya Ini aina ya C kwa asilimia 80 ya watu wanaoihitaji.

WHO inasema eneo la Pasifiki ya magharibi ndilo linaongoza kwa kuwa na watu wengi zaidiwaishio na vidudu vinavyosababisha homa ya Ini katika maeneo sita yaliyoathirika zaidi na homa hiyo duniani.

Hadi mwishoni mwa mwaka 2015, takriban watu milioni14, walikuwa wanaishi na vidudu vya homa ya ini aina ya C huku wengine milioni 155 waliambukizwa aina ya B,  na kila siku watu 1,200 wa eneo hilo hufariki dunia kwa kukosa matibabu ya homa ya ini.