Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkutano wa 71 wa Baraza Kuu la afya duniani wakunja jamvi

Mkurugenzi mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus
UN/Daniel Johnson
Mkurugenzi mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus

Mkutano wa 71 wa Baraza Kuu la afya duniani wakunja jamvi

Afya

Mkutano  wa Baraza Kuu la afya duniani  uliokuwa unaendele mjini Geneva Uswisi umemalizika.

Katika kikao cha mwisho, mkurugenzi mkuu wa shirika la  afya duniani,WHO Dkt  Tedros Adhanom Ghebreyesus, amewaambia wajumbe kuwa wameweka mwelekeo mpya wa shirika hilo. Amesema mpango huo mpya wa miaka mitano hadi 2023 unaitwa billion 3 ukimaanisha kwamba: watu zaidi ya bilioni 1 kufaidika na huduma za afya kwa wote; watu wengine zaidi ya bilioni 1  kulindwa vizuri dhidi ya dharura za kiafya na bilioni 1 wengine watafurahia afya bora pamoja na ustawi nzuri.

Wajumbe pia wamekubaliana kuhusu mkakati wa kukabiliana na masuala ya lishe ya kina mama wajawazito na watoto wachanga

  Wajumbe wamekariri azma yao ya kuwekeza na kuboresha sera na mipango ili kuimarisha lishe kwa watoto.

Na kwa ujumla baraza limeambiwa kuwa kumekuwa na kasi ndogo ya kupunguza kudumaa kwa watoto licha ya kubaini kuwa hatua chache zilifikiwa katika kupunguza idadi ya watoto wa umri  wa chini ya miaka mitano wanaodumaa kutoka milioni 169 mwaka 2010 hadi milioni 151 katika mwaka 2017.

Mkurugenzi Mkuu amekamilisha hotuba yake  kwa kuwaomba wajumbe kuzidisha juhudi zao kwa wananchi akisema watu wanaowahudumia ni watu wa kawaida na wala sio viongozi.