Nishati mbadala ndio dawa mujarabu ya maendeleo Somalia
Idadi ya watu nchini Somalia inaongezeka kwa kasi hususan kwenye maeneo ya mijini hali inayochangia mazingira kuharibiwa kutokana na mizozo na pia matumizi mabaya ya misitu , umesema Umoja wa Mataifa nchini humo. Maelezo zaidi na Flora Nducha
Somalia ambayo imesambaratika kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa zaidi ya miongo miwli sasa ina kiu kubwa ya maendeleo hususan ya viwanda .Hivi sasa miondombinu karibu yote ya nishati inayosukuma gurudumu la maendeleo haiko, sasa debe linapigwa kuhakikisha miundombinu hiyo inafufuliwa na hasa ya nishati mbadala kwani ndio kichocheo cha maendeleo. Mohamud Farah Ali ni afisa mkuu wa masuala ya kiufundi wa kampuni ya Beco inayozalisha umeme utokanao na nishati mbadala .
(SAUTI YA FARAH)
“Nishati mbadala ndio ufunguo, tusipowekeza katika nishati hiyo, inamaanisha hatutaweza kuwekeza katika jambo lolote lile. Angalia hali ya hewa jua tele.Hapa Somalia tuna zaidi ya saa tano za jua kwa siku. Kwa hivyo huo ni uwekezaji muafaka katika nishati mbadala nchini Somalia na ndilo tunalolifanya.”
Somalia inatajwa kuwa ni moja wa mataifa ya Aafrika yenye viwango vya juu vya bei ya umeme ambapo katika mji mkuu Mogadishu kilowatti moja ya umeme inauzwa dola moja kwa saa kwani umeme ni wa Jenereta zinazotumia mafuta mengi. Bw Farah Ali, anahimiza nishati mbadala
(SAUTI YA FARAH)
“Kila tunapowekeza katika megawati 2.5 za nishati ya jua , huwa tunapunguza mapipa 10, 000 ya dizeli, hii ikimaanisha unapunguza hewa ya ukaa kwenye mazingira, kwa hivyo uwekezaji halisi ni wa kuwekeza katika nishati mbadala”.
Naye mkuu wa mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia UNSOM Michael Keating aliyezuri kampuni hiyo ya Beco amesema kuwekeza katika vyanzo vya nishati mbadala na kujaribu kupunguza bei ya nishati ili kuwanufaisha wananchi wa kawaida ni jambo jema ambalo linaweza kusaidia kulinda mazingira na kuleta jamii pamoja.