Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu wabainika Somalia- Ripoti

Wasimamizi wa uchaguzi wahesabu kura wakati wa uchaguzi wa bunge la chini Baidoa, Somalia Novemba 2016.
UN Photo/ Sabir Olad
Wasimamizi wa uchaguzi wahesabu kura wakati wa uchaguzi wa bunge la chini Baidoa, Somalia Novemba 2016.

Ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu wabainika Somalia- Ripoti

Haki za binadamu

Ripoti ya ofisi ya Umoja wa Mataifa ya usaidizi nchini Somalia, UNSOM na ile ya haki za binadamu, OHCHR,  imeweka bayana ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu uliofanyika nchini humo kati ya mwishoni mwa mwka 2016 hadi mwanzoni ma mwaka 2017.

Ukiukwaji  huo umefanywa na vikosi vya usalama vya serikali wakiwemo polisi na maafisa wa usalama wa taifa, vikundi vilivyojihami vya kiraia kikiwemo Al Shabaab.

Miongoni mwa matukio hayo ni mauaji ya viongozi 13 wa koo na wajumbe wawili wa uchaguzi kati ya Agosti 2016 na tarehe 8 Februari wakati wa uchaguzi mkuu wa urais.

Ripoti inasema mauaji yaliendelea hata baada ya kipindi hicho ambapo viongozi wengine 29 wa koo waliuawa pamoja na wajumbe wa uchaguzi wakiwemo wanawake watatu.

Hata hivyo  mpaka sasa ni matukio mawili tu ya mauaji kati ya 44 ndio yamechunguzwa na wahusika kushtakiwa.

Ripoti inasema ukosefu wa usalama, taasisi dhaifu za kusimamia sheria, na kutokuwepo kwa mfumo bora wa kulinda haki za binadamu vimesababisha ukosefu wa uwajibikaji visa vya ukiukaji wa haki za biandamu nchini Somalia

Makundi mengine  yaliyokumbwa na ukiukwaji  huo wa haki ni waandishi habari, watetezi wa haki za binadamu, pamoja na viongozi wa kisiasa.

Ripoti inasema ghasia hizo zilizuia wananchi kupata habari na hivyo kushindwa kufaidika na pia kuchangia katika mchakato wa kidemokrasia katika masuala mengi.

Akizungumzia ripoti hiyo, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia na mkuu wa UNSOM Michael Keating amesema kwa kuzingatia hali ilivyokuwa chaguzi zilizopita, ni vyema serikali ihakikishe kuwa inaweka mfumo bora wa uwakilishi na shirikishi kwa wananchi wote kuelekea uchaguzi wa mwaka 2020-2021.

“Mchakato huo uwe wa mtu mmoja, kura moja,” amesema Bwana Keating  kwa kuzingatia kuwa hivi sasa nchini Somalia wapiga kura wa kumchagua rais ni wajumbe maalum wanaowakilisha wananchi.

Naye kamishna mkuu wa haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Zeid  Ra’ad Al Hussein  amesema wakati Somalia  inaendelea na jukumu zito la kujenga taasisi suala la kuheshimu haki za binadamu ni lazima lizingatiwe.