Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuondoka kundi la LDCs ni faida zaidi kuliko hasara- Gay

Mwanamke mwenye umri mdogo anakagua mchele katika kijiji moja Bangladesh.
UNDP/Jashim Salam
Mwanamke mwenye umri mdogo anakagua mchele katika kijiji moja Bangladesh.

Kuondoka kundi la LDCs ni faida zaidi kuliko hasara- Gay

Ukuaji wa Kiuchumi

Hii leo kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu sera za maendeleo, CDP inatangaza nchi ambazo zimefanikiwa kutoka katika kundi la nchi zilizo katika harakati za kujikwamua kiuchumi, LDCs.

Hii leo kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu sera za maendeleo, CDP imetangaza nchi 4 ambazo zimependekezwa kuondolewa kutoka katika kundi la nchi zilizo katika harakati za kujikwamua kiuchumi, LDCs.

Nchi hizo ambazo ni Bhutan, Kiribati, São Tomé na Principe pamoja na visiwa vya Solomon, zimetangazwa baada ya kukidhi vigezo ambavyo hutumiwa kubaini iwapo nchi bado ni LDCs au la.

Vigezo hivyo ni pamoja na pato la ndani la taifa, hali ya elimu na afya kwa wananchi wake pamoja na uchumi stahimilivu.

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa pamoja na lile la masuala ya uchumi na kijamii, ECOSOC ndiyo yenye mamlaka ya kuridhia au kukataa mapendekezo ya nchi kuondolewa katika orodha ya LDCs.

Jose Antonio Ocampo ambaye ni mwenyekiti wa kamati hiyo ametaja nchi nyingine ambazo zimependekezwa ili baadaye ziondolewe kwenye orodha hiyo kuwa ni Nepal, Timor Letse na Bangladesh. Amesema kuendelea kuboreshwa kwa huduma za afya na kijamii ni kichocheo kwa nchi kuondolewa katika orodha ya LDCs.

Akizungumzia mwelekeo huo, Daniel Gay ambaye ni mshauri wa kikanda katika kamati hiyo amejibu hoja ya kwamba baadhi ya nchi huwa na hofu ya kuondoka katika kundi hilo kwa kuwa kwa kufanya hivyo wanakosa misaada na unafuu kwenye biashara.

(Sauti ya Daniel Gay)

“Ni kweli baadhi ya nchi huhofia kuwa watakosa manufa ya biashar na misaada lakini nchi nyingine zinaona ni jambo bora zaidi badala ya kutegema biashara na misaada. Mfano Bangladesh kwa mara ya kwanza mwaka huu imekidhi vigezo vyote vitatu na wana shauku kubwa ya kuondoka kwenye kundi la nchi maskini kwa sababu wanafikiri hiyo ni ishara ya maendeleo. Ni miaka 50 tangu ipate uhuru na wanaona maendeleo yamekuwa ya kasi sana katika miaka michache iliyopita.”

Na zaidi ya yote Bwana Gay ametaja faida za kuondoka kwenye kundi hilo kuwa ni ..

(Sauti ya David Gay)

“Wanataka kuvutia vitegauchumi zaidi na wanafikiri kuwa kwa hadhi yao kuinuka, itaruhusu wao kutambulika kimataifa kuwa ni eneo bora zaidi la uwekezaji na kupata mtazamo kuwa ni mshiriki muhmu katika ngazi ya kimataifa.”

Kipengele cha nchi zilizo katika harakati za kujikwamua au nchi maskini, LDCs kilianzishwa mwaka 1971 ambapo hadi sasa kuna jumla ya nchi 47. Kati ya hizo 33 ziko Afrika, 13 Asia na Pasifiki ilihali Amerika  ya Kusini ni 1.

Tangu mwaka 1971 ni nchi tano tu ambazo zimefanikiwa kuondoka katika orodha na miongoni mwao ni Botswana na Maldives.