Kuna alama za mauaji ya kimbari Myanmar-UN
Kuna dalili za mauaji ya kimbari katika mkoa wa Rakhine dhidi ya warohingya.Hayo yametamkwa na mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu nchini Mynamar, Yanghee Lee, wakati akilihurubia baraza la haki za binadamu jumatatu mjini Geneva
Akifafanua hilo amesema kuwa kwa maoni yake anahisi kuwa matukio katika mkoa wa Rakhine, unaopatikana nchini Myanmar, yana alama za mauaji ya kimbari na kutaka kuwepo uwajibishwaji.
Mwaka jana Lee alizuiliwa kuingia nchini Myanmar, na leo jumatatu ametoa wasiwasi wake kuwa huenda vitendo vya ukandamizaji vya serikali za kijeshi zilizopita ndio vinarejea nchini Myanmar, akieleza kama hali inayoyakabili makundi ya kiraia nchini humo ni ya kuhatarisha.
Lee ametaka kufanyika kwa uchunguzi wa kina na wa haraka bila kuchelewa na wahusika wachukuliwe hatua dhidi ya makosa yanayodaiwa kufanyika katika mkoa wa Rakhine kuanzia tarehe Oktoba mwaka 2016 na Agosti 25 mwaka 2017, pamoja na fujo zinazoendelea hadi sasa.
Ameongeza kuwa dunia sasa imejikita na mgogoro wa mkoa wa Rakhine na kupuuza ghasia katika mikoa ya Kachim, Shan na pia mikoa mingine nchini Myanmar ambayo imeathirika na machafuko kama hayo.