Ahsante Malaysia na Indonesia kwa kuwakoa warohingya-UNHCR
Shirika la kuwahudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa la UNHCR huku likitoa shukurani kwa baadhi ya mataifa jirani na Myanmar kwa kuwahurumia na kuwasaidia warohingya wanaotoroka makwao kwa upande mwingine, linasema linawasiwasi kutokana na taarifa za baadhi ya wakimbizi waliowasili juzi wakitumia mashua kuwa walisumbuliwa wakiwa njiani.
UNHCR inasema visa kama hivyo sio tu vinaweka maisha ya wakimbizi katika hatari lakini pia vinakwenda kinyume na sheria za kimataifa kuhusu usafiri wa majini.
Mkuu wa UNHCR kanda ya Kusini Mashariki mwa Asia, James Lynch, amesema ili kuepuka kupoteza tena maisha anaziomba serikali zote katika eneo hilo kufuata sheria za usafiri wa majini na mwoyo wa tamko la Bali la mwaka 2016, la kuwaokoa wakimbizi kwa kuwashusha katika maeneo salama ya karibu na kujizuia kufanya mambo ya kuwasimamisha ndani ya bahari hali ambayo yaweza kuhatarisha maisha yao.
Tena kuhusu shukrani, inahusu visa vya wanausalama wa Indonesia na Malaysia kuokoa mashua tatu zikiwa zimebeba watu 140, wote wakimbizi wa Rohingya waliotoroka Myanmar mwezi Aprili kupitia majini. Wakimbizi hao sasa wako salama na wa afya bora.
Taarifa za awali zasema takriban wakimbizi 10 walitokomea majini. Tangu mgogoro huu mpya uanze, Agosti 2017, watu 200 na ushei wanakadiriwa kutoweka katika eneo la ghuba ya Bengali sanasana wakiwa wanavuka kutoka Myanmar hadi Bangladesh.
Mashua hizo tatu zilitoka jimbo la Rakhine nchini Myanmar na ni wakimbizi wa kwanza waRohingya wanaotumia usafiri wa maji kuhakikishwa kutumia njia ya bahari ya Andaman tangu Mei 2015.