Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Asia-Pasifiki yalenga maendeleo jumuishi na endelevu ya viwanda

Asia-Pasifiki yalenga maendeleo jumuishi na endelevu ya viwanda

Mchango wa maendeleo jumuishi na endelevu ya viwanda katika ajenda ya maendeleo baada ya 2015 umemulikwa leo katikaa kongamano la Asia-Pasifiki kuhusu maendeleo endelevu, ambalo limeandaliwa na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu uchumi na jamii Asia na Pasifiki, mjini Bangkok,Thailand.

Washiriki kwenye mjadala huo wamesisitiza umuhimu wa ukuaji wa viwanda kwa uendelevu wa shughuli za kiuchumi na kuendeleza ujumuishaji wa kijamii, ambavyo tayari vimetambuliwa katika mapendekezo ya malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.

Hata hivyo, baadhi ya washiriki kwenye mjadala huo wamekumbusha kwamba ukuaji wa viwanda na utajiri uliotokana nao haujawanufaisha watu wote kwenye ukanda wa Asia-Pasifiki, na kwamba maendeleo ya viwanda kwenye ukanda huo umekuwa na gharama ya kuathiri mazingira.

Wamekubaliana kuwa, ili kupunguza umaskini, kuendeleza usawa na kugawana mafanikio ya maendeleo kwa jamii zote, viwanda vinapaswa kukua kwa njia jumuishi na endelevu.