Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kenya tunga sera zinazochochea ongezeko la ajira:ILO

Kenya tunga sera zinazochochea ongezeko la ajira:ILO

Shirika la kazi duniani , ILO limefanya utafiti kuhusiana na masuala ya ajira nchini Kenya na kubaini kuwa nchi hiyo yahitajika kuridhia mkakati wa kitaifa wa ajira utakaotoa fursa sawia za ajira kwa makundi yote ikiwemo vijana. Taarifa zaidi na Grace Kaneiya.

(Taarifa ya Grace Kaneiya)

Utafiti huo wa ILO unaonyesha kuwa licha ya kiwango cha ukuaji wa uchumi nchini Kenya kuendelea kukua mwaka hadi mwaka, bado matokeo hayo hayako bayana katika maisha ya kila siku ya vijana.

Mathalani ajira kwa vijana imebakia kuwa tatizo ambapo mwaka jana asilimia 35 ya watu wenye uwezo wa kufanya kazi walikuwa vijana wenye umri wa kati ya miaka 15 na 24 lakini kati yao ni asilimia Tisa tu waliokuwa na ajira.

Verónica Escudero mchumi wa ILO ambaye ameshiriki kuandaa ripoti hiyo anasema kudorora kwa vijana kushiriki kwenye ajira kutakwamisha hatma ya ukuaji wa uchumi wa nchi hiyo kwa siku za usoni.

Ili kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana, ripoti hiyo imependekeza hatua tatu ikiwemo mpango wa kitaifa ambao utaunganisha masuala ya ajira na uchumi wa taifa, kuweka mazingira bora ya uwekezaji na kuendeleza fursa za ajira zenye utu hususan kwenye sekta isiyo rasmi.