Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO na washirika wake wameanza kuwafikia wanaohitaji msaada katika visiwa vingi Ufilipino:

WHO na washirika wake wameanza kuwafikia wanaohitaji msaada katika visiwa vingi Ufilipino:

Shirika la afya duniani WHO linafanya kazi kwa karibu na serikali ya Ufilipino na wadau wengine wa kimataifa kuwafikia manusura wa kimbunga Haiyan ambao wanahitaji huduma za afya.

Hali halisi ya athari za kimbunga hicho inaanza kubainika sasa huku maeneo mengi yakihitaji msaada. Takribani majimbo saba yameathirika na kimbunga hicho ambayo ni Samar, Leyte, Cebu, Iloilo, Capiz, Aklan and Palawan na kituo cha misaada ya kibinadamu kimeweka katika kila jimbo hivi sasa.

Kuna hofu kwamba visiwa vingine vidogovidogo 20 katika maeneo ya vijijini vinaweza kuwa vimeathirika na kimbunga hicho hali ambayo ni changamoto kubwa kufikisha msaada. Mfumo wa afya umeathirika vibaya khuku vituo 18 kati ya 38 vya afya vimesambaratishwa kabisa lakini huduma sasa imeanza kufika kwa wahitaji.

Timu ya wataalamu 50 wa WHO ipo Ufilipino kuisaidia serikali kushirikiana na wauguzi na madaktari ambao tayari wapo nchini humo. Inakadiriwa kuwa kuna wanawake 200,000 wajawazito na 130,000 wanaonyonyesha wako katika maeneo yaliyoathirika vibaya.