Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Naibu Kamishna wa haki za binadamu wa UM kuzuru DRC

Naibu Kamishna wa haki za binadamu wa UM kuzuru DRC

Naibu Kamishna wa Tume ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Flavia Pansieri baadaye wiki hii ataanza ziara ya wiki moja huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kama anavyo ripoti Grace Kaneiya.

 (RIPOTI YA GRACE KANEIYA)

Wakati wa ziara yake Pansieri atakutana na maafisa wa serikali ya DRC wakiwemo wale wa ngazi za juu jeshini pamoja na mahakama. Pansieri pia atafanya mazungumzo na waakilishi kutoka kwa mashirika ya umma na mashirika tofauti kutoka Umoja wa Mataifa yanayoshughulika na masuala ya haki za binadamu nchini humo.

Naibu kamishina mkuu atazuru mashariki mwa DRC kutathmini hali ya haki za binadamu pamoja na kazi inayofanywa na ofisi hiyo tangu kutumwa kwa kikosi cha Umoaja wa Mataifa cha kulinda amani eneo hilo MONUSCO.

Pansieri atazungumzia masuala ya kukabiliana na ukwepaji wa sheria na kuwalinda raia kupitia ushirikiano kati ya Umoja wa Mataifa, serikali ya DRC na mashirika mengine yasiyokuwa ya serikali. Baadaye atasafiri kwenda maeneo ya Masisi na Mambasa ambapo atafanya mazungumzo yanayoangazia dhuluma za kimapenzi.