Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Papa Francis awaombea wahamiaji na wakimbizi kwenye kisiwa cha Lampedusa

Papa Francis awaombea wahamiaji na wakimbizi kwenye kisiwa cha Lampedusa

Papa Francis, kiongozi wa Kanisa Katoliki ametoa wito kuwepo uelewa na kuungana kwa ajili ya maelfu ya watu ambao huhatarisha maisha yao kila mwaka wakijaribu kuvuka bahari kwenda Uropa na kuwaombea wale ambao wamepoteza maisha yao wakijaribu kufanya hivyo. Papa Francis amesema hayo wakati wa ziara yake kwenye kisiwa cha Lampedusa, Italia leo Jumatatu.Saa chache kabla ya kuwasili kwake, boti moja ndogo ilowabeba watu 166 kutoka nchi tofauti iliwasili kwenye kisiwa hicho kilichoko kilomita 120 kutoka Tunisia. Walinzi wa pwani ya Italia waliripotiwa kuiokoa boti nyingine ilowabeba watu 120 mnamo siku ya Jumapili, akiwemo mama mja mzito.

Mwakilishi wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi katika Umoja wa Mataifa, UNHCR kwenye ukanda huo, Laurens Jolles, amesema ziara ya Papa Francis ni yenye thamani kubwa ya kibinadamu, na kumsifu kwa jinsi ambavyo ameonyesha kuwazingatia wakimbizi na wahamiaji katika miezi yake ya kwanza kama Papa.

UNHCR inakadiria kuwa takriban wahamiaji na watafuta hifadfhi 8, 400 waliwasili kwenye pwani ya Italia katika miezi sita ya kwanza pekee mwaka huu. Wengi wao walitoka barani Afrika, katika nchi za Somalia na Eritrea, lakini pia wengine hutokea nchi za Afghanistan, Misri, Gambia, Mali, Pakistan na Syria.