Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR yataka fedha kuwahudumia wakimbizi wa Mali

UNHCR yataka fedha kuwahudumia wakimbizi wa Mali

Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na wakimbizi UNHCR limetoa wito wa kuongeza mafungu ya fedha kwa ajili ya kugharimia usambazaji wa mahitaji muhimu wa maelfu ya wakimbizi wa Mali na wale waliokosa makazi.

Shirika hilo limesema kuwa linahitaji kiasi cha dola za Marekani milioni 144 kwa ajili ya kufanikisha mipango yake ya kuwahudumia wakimbizi hao.

Lakini hadi sasa limepokea kiasi cha asilimia 32 hatua ambayo inafanya utekelezaji wa majukumu yake kuwa mgumu.

UNHCR inakusudia kuendesha upanuzi wa kambi pamoja na kuimarisha hali ya utoaji wa huduma muhimu ikiwemo chakula na makazi.

Kwa sasa kuna zaidi ya wakimbizi 175,000 wanaendelea kumiminika katika nchi za jirani, ikiwemo wakimbizi 75,850 waliko nchini Mauritania na wengine 50,000 ambao wameomba hifadhi katika nchi jirani ya Niger.