Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ongezeko la ghasia linaathiri watu Iraq, yaonya mashirika ya usalama ya UM

Ongezeko la ghasia linaathiri watu Iraq, yaonya mashirika ya usalama ya UM

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Iraq umeelezea wasi wasi wake kuhusu ongezeko la ghasia katika  nchi hiyo ya Mashariki ya kati ambako takriban zaidi ya raia 200 wamepoteza maisha huku zaidi ya watu 800 wakijeruhiwa katika kipindi cha mwezi mmoja tu.

Afisa mkuu wa haki za binadamu katika ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini Iraq (UNAMI) Francesco Motta, amesema wanachukizwa na kupoteza kwa maisha ya raia kufuatia vitendo vya ugaidi na mizozo ya makundi yaliyojihami.

Halikadhalika wanasikitishwa na ongezeko la idadi ya askari ambao kila siku wanaitwa ili kushiriki katika vikosi vya kukabiliana na ghasia, ugaidi, ulinzi wa raia na miundombinu.

Ghasia zimeathiri maandalizi ya chaguzi ndogo zitakazofanyika tarehe Aprili 20. Mathalani wagombea 10 waliokuwa katika kinyang’aniro hicho wamekufa na hivyo kulazimu baraza la mawaziri nchini Iraq kuahirisha uchaguzi katika maeneo ya Anbar na Ninewe kwa muda wa hadi miezi sita kutokana na hofu ya usalama.