Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanawake zaidi wajawazito na watoto ni lazima wapate matibabu ya Ukimwi: UNICEF

Wanawake zaidi wajawazito na watoto ni lazima wapate matibabu ya Ukimwi: UNICEF

Maambukizi mapya ya virusi vya HIV miongoni mwa watoto yamepunguwa, lakini kulifikia lengo la kuwa kizazi kisicho na Ukimwi kunahitaji kuwatibu wanawake zaidi waja wazito na watoto, ambao wanaishi na virusi vya HIV, limesema Shirika la Kuhudumia Watoto katika Umoja wa Mataifa, UNICEF, katika ujumbe wake kabla ya siku ya Kimataifa ya Ukimwi, Disemba mosi.

Kwa sababu ya kujitolea kwa njia ya kipekee, ulimwengu umeshuhudia kushuka kwa viwango vya maambukizi mapya ya HIV miongoni mwa watoto kwa asilimia 24, kutoka laki nne na thelathini elfu mwaka 2009, hadi laki tatu na thelathini elfu mwaka 2011.

Kufikia Disemba mwaka 2011, watoto laki moja zaidi walikuwa wanapokea matibabu ya dawa za kupunguza makali ya HIV, ikilinganishwa na mwaka wa 2010. Hata hivyo, chini ya thuluthi moja ya watoto na akina mama wajawazito wanapata matibabu wanayohitaji, ikilinganishwa na kiwango cha kimataifa cha asilimia 54 ya watu wazima kwa jumla, hali ambayo mkuu wa UNICEF, Anthony Lake ametaja kuwa isiyokubalika.