Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wachunguza usafirishaji haramu wa binadamu Ufilipino

UM wachunguza usafirishaji haramu wa binadamu Ufilipino

Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa limemtuma mtaalamu huru kuhusu masuala ya usafirishaji haramu wa binadamu kwenda nchini Ufilipino kuchunguza hali halisi usafirishaji haramu wa binadamu nchini humo na athari za mikakati ya kupambana na vitendo hivyo.

Mtaalamu huyo Joy Ngozi Ezielo ataanza ziara hiyo tarehe Tano mwezi huu hadi tarehe Tisa ambapo amesema ni matumaini yake kusikia maoni na kujifunza kutoka kwa watu waliosafirishwa kinyume cha sheria na watu wengine ambao wanakabiliana na vitendo hiivyo ili kuhakikisha kuwa jitihada zote za kuvizuia vinazingatia haki za binadamu.

Ziara hiyo ya Bi. Ezielo itamfikisha mji mkuu Manila pamoja na Zamboanga na Cebu ambapo atajadiliana na maafisa wa serikali ya Ufilipino na wadau wengine wakiwemo maafisa wa mahakama, mashirika yasiyo ya kiserikali na  yale ya kimataifa kuhusu mafanikio na changamoto za jitihada za kupambana na ainazote za kusafirisha binadamu kinyume cha sheria nchini humo.

Mapendekezo yatokanayo na ziara hiyo yatawasilishwa wakati wa kikao kijaho cha Baraza la Haki la Binadamu la Umoja wa Mataifa.