Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban alaani mashambulizi ya kigaidi Syria

Ban alaani mashambulizi ya kigaidi Syria

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amelaani vikali tukio la shambulizi la kigaidi katika mji wa Idlib na mlipuko wa bomu iliyojiri katika mji mkuu wa Syria Damascus ambayo yamesabisha watu kadhaa kupoteza maisha na wengine kujeruhiwa.

Akielezea hali hiyo, Ban amesema kuwa anasalia kuwa mtu mwenye huzuni na uchungu mkubwa kutokana na kuendelea kujiri kwa matukio ambayo yanakwamisha uhai wa raia na uvunjivu wa haki za kimsingi.

Duru za vyombo vya habari zinasema kuwa watu kadhaa walipoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya wakati wa mlipuko huo uliojiri wiki iliyopita katika viunga vya mji mkuu Damascus.

Tangu kuanza kwa machafuko nchini humo March 2011, kiasi cha watu 9,000 wanaripotiwa kufariki dunia na idadi kubwa ya watu wakijeruhiwa na wengine kulazimika kukimbilia uhamishoni.