Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban anaishukuru Uruguay kwa mchango wake kwenye vikosi vya kulinda amani

Ban anaishukuru Uruguay kwa mchango wake kwenye vikosi vya kulinda amani

 

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon aliyeko ziarani Uruguay ameipongeza na kuishukuru nchi hiyo ya Amerika ya Kusini kwa mchango wake mkubwa wa mipango ya Umoja wa Mataifa ya ulinzi wa amani. Ban amesema licha ya idadi ya watu wa nchi hiyo Uruguay inashika nafasi ya kwanza duniani kwa kuchangia katika mipango ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa.

Na kwa sasa Ban amesema Uruguay inachukua nafasi ya pili kwa kutoa vikosi vingi kwenye mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Haiti MINUSTAH ambao pia uko kwenye eneo la Amerika Kusini.

Ban pia amegusia suala la uzalishaji na kujivua silaha za nyuklia ambapo amesema taifa hilo limekuwa msitari wa mbele katika kutekeleza mikataba ya Umoja wa Mataifa. Ban ambaye anazuru kwa mara ya kwanza katika taifa hilo amesema wiki ijayo Uruguay itaanza jukumu la kuwa Rais wa baraza la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambapo kwa mara ya kwanza kabisa, baraza hilo litakuwa na Rais mwanamke. Amelitaja taifa hilo kuwa ni mfano wa kuigwa katika mambo mengi.

(SAUTI YA BAN KI-MOON)

Ban ameongeza kuwa anaamini eneo zima la Amerika ya Kusini linaweza kuwa na jukumu hata kubwa zaidi kwenye Umoja wa Mataifa na vivyo hivyo Umoja wa Mataifa katika eneo hilo.