Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mpango wa amani nchini Nepal wakumbwa na utata:Ban

Mpango wa amani nchini Nepal wakumbwa na utata:Ban

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki moon amesema kuwa mpango wa amani nchini Nepal unaendelea kukumbwa na utata huku Umoja huo ukijiandaa kuondoka nchini humo.

Ban anasema kuwa changamoto kuu kwa sasa ni kuwabadili wapigani wa kundi la Mao ambao walipigana vita vya muongo mmoja vya wenyewe kwa wenyewe. Ban amesema kuwa kuna masuala yanayoeweza kuzua mzozo upya na kutoa wito kwa pande husika kuchukua hatua zinazohitajika na kuyapa kipaumbele masuala ya nchi yaliyo muhimu.

Katika ujumbe kwa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa Ban amesema kuwa hatua zinastahili kuchukuliwa ili kuwabadili wapiganaji wa kundi la Mao kwa njia inayofaa akiongeza kuwa si vyema Umoja wa Mataifa kuondoka na kuacha pengo.

Ban anasema kuwa hata baada ya serikali na kundi la Mao kuafikiana mwezi Septemba mwaka 2010 kuwa yaliyosalia kwenye mpango huo wa amani yatekelezwe mwezi Januari mwaka 2011 bado hakuna hatua zilizopigwa.